Monday, March 20, 2023

Ukifanya hiki utajitoa kwenye mazoea

Imekuwa kasumba kwa wengi wetu hasa mahali pa kazi kukwepa baadhi ya majukumu. 

Wakati mwingine unaenda katika ofisi fulani, ukitaka kupewa huduma fulani. Mhusika unayekutana naye, anakwambia nenda meza ile huyo atamaliza shida yako. 

 Unapochukua hatua ya kwenda kwa huyo mtu uliyeelekezwa labda ni IT au customer care badala amalizie shida yako anakwambia subiri kesho au kesho kutwa kuna mfumo haupo sawa. 

Pengine hamna shida yoyote, amejisikia uvivu tu. Hii hali imekuwa inarudisha nyuma maendeleo yetu kwa kiasi kikubwa. 

Unaenda kwa fundi anakwambia njoo baada ya siku mbili. Ukienda anakwambia umeme ulikata njoo keshokutwa. Ukija anakwambia kuna kifaa kakiagiza mahali. Huo wote ni uvivu tu wa kufanya kitu chako. 

Hii hali inapoendelea kuna watu wanaanza kujitoa taratibu taratibu kwenye biashara au huduma yako. Kwa sababu hakuna kitu wateja au watu wanakwepa kama kuzungushwa mara mbili au tatu. Ukimfanyia hivyo jua umempoteza. 

Ili tuwafanye wathamini huduma zetu, tuache uvivu kama kazi imekuja kwako ifanye kwa moyo wote. Muheshimu aliyeacha kazi zake akaja kwako umfanyie kazi. 

Kama ingekuwa halipi pesa yake sawa. Lakini wanalipa pesa ndicho kinachoumiza moyo. Pesa inatafutwa kwa shida. Hivyo, ukiiheshimu na ukaipokea kihalali watakuheshimu na kukupa kazi nyingi. 

Lijue hili likusaidie kukuza brand yako. Acha uvivu fanya kile kinachowezekana. 

Una changamoto yoyote bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert
Hamasika 2023

Saturday, March 18, 2023

Usichoke, ndiyo maisha yetu


Kauli isemayo ukifaulu mtihani mmoja kwenye maisha usiwadharau waliofeli ni kweli kabisa. Kwa sababu maisha yanayo mitihani mingi sana. 

Unamaliza mmoja, unakuja mwingine zaidi yake. Unakumbuka siku umebanwa na kodi ya nyumba. Ukaumiza kichwa sana kuitafuta ili uendelee kulala chumbani kwako kwa raha mstarehe. Ile umemaliza kuilipa hivi, ukaambiwa mama anaumwa inatakiwa pesa ya matibabu. 

Ile furaha na amani uliyokuwa unaitegemea ilipotea ghafla. Pengine ukajisemea hii pesa inanipa furaha bandia. Nimekamilisha moja limekuja jingine. 

Umemaliza elimu ya chuo kikuu, ukiwa na dhana ya kwamba maisha umeyaweza. Hakuna kingine cha kukupa shida. Mara unakutana na janga la ukosefu wa ajira. Huu ni mtihani mwingine mkubwa. Unaanza kupigana nao. 

Umefanikiwa kuingia kwenye ndoa ukasema sasa mateso basi. Amani, furaha na starehe vinaanza. Majukumu yanapoanza kuwa mengi unajiuliza wapi pa kupumulia. Mke anataka hitaji hili, mtoto anataka hitaji lingine. Ndiyo maisha yetu. 

Pengine, umefanikiwa kununua gari ukasema; kuninginingia kwenye daladala basi. Ulipoipeleka garage gharama za vifaa na mafuta jasho linaanza kukutoka. Mawazo mengi juu ya services zake. Ndiyo maisha yetu ndugu. 

Sasa unafanya nini katika hali hiyo. Ni kitu kimoja unachohitaji na kitu hicho ni maandalizi. 

Uzuri wa kuwa na maandalizi katika kila kitu unachofanya yanakusaidia kupunguzwa uwezekano wa kushindwa. Ndio maana upo msemo wa wakati wa vita sio wakati wa kujiandaa. Bali kabla ya vita ndiyo wakati sahihi wa kujiandaa. 

Hata kwenye maisha yetu ndivyo ilivyo. Unahitaji kuwa na maandalizi ya kutosha kabla hujaanza kufanya kitu. Maisha yanatufundisha kila siku na mitihani tunayofanya ni majukumuku na kazi zetu za kila siku. 

Usiache kujiandaa na mambo yataenda vema. 

Una changamoto yoyote bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
Hamasika2023

Friday, March 17, 2023

Nini kinafanya wakuchague?


Siku moja nilialikwa na taasisi moja kwa ajili ya kusimamia zoezi la usaili wa kazi. Kwenye jopo tulikuwa watu wanne . Kwa sababu mimi ni mtaalamu katika masuala la Sheria za Kazi na Ajira. Walinipa nafasi kubwa na wote walikuwa wanasikiliza neno la mwisho kutoka kwangu. 

Usaili kiukweli ulienda vizuri, nikiwa makini sana kuhakikisha anapatikana mtu sahihi. 

Wakati tunaendelea na usaili kuna dada mmoja tumuite Mwajuma japo sio jina lake halisi aliingia akaanza kujielezea background ya elimu na ujuzi wake. 

Kikafika kipindi cha maswali nikamuuliza swali la kwanza. Je, unajua nini kinafanya tukuchague wewe? 

Mwajuma akasema, ni Kwa sababu mkinichagua nitaweza kumsaidia baba yangu anayeumwa nyumbani. Matibabu yatatokana na mshahara mtakaonilipa. 

Nilimwambia tumekusikia. Nikashika kichwa na kujiuliza maswali mengi. Je, huyu anajua anachofanya? Na hiki alichosema anakijua au amesahahu kwamba  hakuna mtu anayekupa kazi kama msaada. 

Baadaye wakata tutoe hitimisho juu ya usaili mzima. Binafsi nilimwambia bosi kwamba mtu pekee mwenye sifa alikuwa ni mmoja tu Mwajuma. Ila tatizo ni moja. Ajajua ni kwa nini anatafuta kazi. 

Kwa hiyo either mtangaze upya au mchukue Mwajuma kisha muelekeze namna bora ya kufanya kazi. Mwambie hupewi kazi kwa sababu ya matatizo uliyo nayo au kama msaada bali ujuzi na namna unavyoweza kuisaidia taasisi kuzalisha zaidi. 

Note: Ukiwa unaomba kazi mahali popote pale, elezea namna utakavyofanya kazi hiyo kwa ufanisi, uadilifu na faida utakayoongeza. Na sio unavyotaka kutatua matatizo yako kupitia kazi.

Usiseme  nina mtoto mdogo na hakuna wa kunisaidia. Ninataka kujikimu kimaisha. Baba yangu anaumwa au mama yangu au kwa sababu nipo tu nyumbani.

Waambie ninaweza kufanya 1, 2, 3 na nipo tayari kufanya kazi kwa jitihada zote ili kuhakikisha kampuni au biashara hii inafikia hatua nzuri.

Sehemu nyingi za kazi wanatafuta wafanyakazi wanaoenda kuleta suluhu na sio kuongeza matatizo. Ikiwa umepata nafasi, usiichezee tena umefika kwenye usaili wa kuongea. Hupaswi kutia doa. 

Funguka onyesha ujuzi wako, hadi wanaofanya usaili washangae. Hii itafanya waone kitu cha ziada kwako. 

Waonyeshe namna unavyoenda kukuza uzalishaji katika kampuni au taasisi husika. Itakutofautisha na wengine. 

Umewahi kukataliwa mahali kisa huna vigezo, ulijua kwa nini? 
Bonga nasi hapa hapa 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
Hamasikaacademy2023

Thursday, March 16, 2023

Nguvu ya jina la kwanza

Helow! Robert, habari yako? 
Helow Lackius, habari yako? 

Hawa ni watu wawili tofauti wanaopiga simu kwa wakati tofauti. Ila attention inachukuliwa na kwa mtu wa pili. Unataka kujua kwa nini? 

Kuna nguvu kubwa ya kutaja jina la kwanza la mtu. Inaonyesha kabisa unamfahamu. Hata kama umepewa namba na mtu ila akakupatia majina mawili, ukitaja jina lake la kwanza. Kuna umakini mkubwa unautengeneza kwake. Mtu aliyepigiwa anaitwa Lackius Robert. 

Ipo hivi sauti ambayo mtu anapenda kuisikia mara nyingi ni jina lake. Hata kama yupo sehemu yenye kelele kubwa, ila akisikia jina lake lazima aweke umakini mkubwa. Hii ni kwa sababu ndiyo sauti anayopenda kusikia. 

Unapokuwa umetaja jina la pili, anakuwa na wasiwasi ikiwa unamjua vema. Anaweza kuhisi kuna umakini fulani unaukosa. Sio kwamba hawezi kuendelea kukusikiliza ila unapokuwa umetaja jina la kwanza anaongeza umakini mkubwa. 

Ukitaka kujua hili, piga simu kwa mtu uliyepewa namba yake akiwa mpya. Anza kutaja jina lake la kwanza utaona namna atakavyoruhusu mazungumzo yenu. 

Wewe timiza hili, taja jina lake la kwanza mara zote unapoongea na mtu. Iwe ni mteja, rafiki au mtu mwingine, usiache kumuita jina lake la kwanza. Ndio siri kubwa iliyofichwa kwenye jina la kwanza. 

Kingine cha kuzingatia ni kutaja jina lake kwa ufasaha zaidi. Epuka kukosea jina la mtu wakati wa kulitaja. Mfano anaitwa Lackius. Epuka kutumia Lackilius utaondoa umakini wake ataona ujali na huna umakini hata kidogo. 

Unapata changamoto yoyoye bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
Mwangaza 2023

Monday, March 13, 2023

Unaweza kushinda mchezo wowote

Napoleon Hill kwenye kitabu chake cha "Think and Grow Rich" anasema "washindi kwamwe hawaachi kufanya". 

Hii kauli inatosha kukupa nguvu na imani kuwa unaweza kuwa mshindi katika mchezo wowote. Iwe mpira, biashara, muziki au kitu kingine. 

Ikiwa unacheza mpira, kama utaendelea kufanya mazoezi bila kuacha. Kujifunza mbinu mpya na kuwa na nidhamu bora hakuna namna utashindwa kufunga magoli mengi zaidi. 

Upo kwenye biashara, ushindi wako ni mauzo. Maana kupitia mauzo ndipo pesa hupatikana. Ushindi huo unaenda kuupata pale ambapo utaamua kufanya endelevu bila kuacha. Unajifunza mbinu mpya za masoko kila siku. Hapo lazima uuze na mchezo wa mauzo kwako itakuwa raha maana utakuwa ni mshindi. 

Upo kazini, ikiwa utaonyesha kujali, kujituma, kuwa na nidhamu na kumaliza kazi kwa wakati. Lazima uwe mshindi katika kazi zako. Maana kupitia nidhamu utajiboresha na kukamilisha kazi zako kwa muda muafaka. 

Ushindi ninaozungumza hapa sio tu wa goli kusema wachezaji ndio wanaostahili kushinda la asha! Ni ushindi katika kazi zako. 

Hawajibu message piga simu. Hawajapokea simu watembelee. Mara zote hakikisha kuna kitu kikubwa unakifanya ukilinganisha na hapo awali. 

Mwanamziki piga kazi zaidi. Jifunze na andaa muziki wenye maadili ili watu wote waweze kupata ujumbe. Kuwa mvumilivu usikate tamaa haraka sana. Ushindi kwenye mziki ni wako. Endelea kuonyesha juhudi kubwa. 

Changamoto ni nyingi tunapitia, wewe fanya tu, timiza wajibu wako kufanya. Kama ni simu 20 wewe piga, kama ni kuwatembelea watu 10 kwa siku ili uwauzie wewe nenda. Kama ni mazoezi wewe nenda. 

Hakikisha mara zote, unakuwa kazini. Fanya bila kuchoka. Unaambiwa mchumia juani ulia kivulini. Wakati ndio huu ushindi wako unakaribia. Kila lakheri.

Je, ni nini kinakukwamisha  ushindi wako kwenye kazi zako? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
Karibu sana tujifunze zaidi. 

Saturday, March 11, 2023

Mabadiliko yanaanza na wewe


Kama kitu kimetengenezwa kinaweza kubadilishwa. Kama kitu kina uhai kinaweza kubadilika kwa hali fulani fulani. 

Chukulia mtoto mdogo anapozaliwa, haanzi kuongea, kutembea au kuwa na meno. Kadiri muda unavyokuwa unasogea ndivyo anavyokuwa anabadilika mdogo mdogo. 

Chukulia mti wa Mbuyu, mwanzoni huwa unaanza kama mchicha. Wakati huo umbo likiwa dogo sana kadiri muda unavyokuwa usogea ndivyo hubadilika pia. Hadi kuwa na umbo kubwa. Ukiambiwa ulikuwa katika umbo dogo unaweza usikubali lakini huo ndio ukweli. 

Ipo hivyo kwenye maisha yako. Hutaweza kubadili mwili au kujiongezea kiungo kingine kwa maana ya mkono wa watatu au mguu wa tatu la asha! Namaanisha unaweza kuibadili hali ya sasa kuwa bora zaidi. 

Huwezi kuibadili jana ila unaweza kuitumia leo kuiboresha kesho yako. Mabadiliko yote haya yanaanza na wewe mwenyewe. Kukubali kuwa kuna mahali unataka kufika. Kuna kitu unataka kukipata katika maisha yako. Kuna hatua kubwa unataka kuipiga. 

Huo ndio ukweli ninaotaka uweze kuujua "any changes starts with you" mabadiliko yoyote yanaanza na wewe. 

Unataka kubadilika kifikra, kimawazo, kimtazamo na kihisia pia. Hii itakusaidia kuwa tayari kutimiza wajibu wako. Kumaliza kile ulichokianza, bila kujali ugumu kiasi gani unapitia. 

Matumaini unayotaka kuwa nayo. Kuwa tayari kupata habari zaidi. Usipoamua kufanya kitu tambua kuwa wewe ndiye muongozaji katika njia yako. Mafanikio unayotaka yanaanzia kwenye akili yako. Unapaswa kuwa tayari kubadilika kimwili na kiroho pia. 

Ni mengi unahitaji kufanya, wakati ndio huu kuyafanya. Hakuna wa kukuzuia kuyafanya. Ni wewe tu kukubali kubadilika na mabadiliko ya kweli unayotakiwa kuyapata yaanzie akilini mwako. Namna unavyoishi kuwa mtu mwenye focus, weka lengo kutimiza malengo. 

Hiyo yote ukiifanikisha amini maisha yako yatabadilika. Usijali kuhusu muda. Wewe jali juhudi unazoweka kuendana na mabadiliko hayo. 

Kumbuka, Umri sio shida. Kipato chako, mahali unapoishi vyote hivyo havina shida. Ukitaka kubadili chochote anza na wewe. Usikimbilie kutoa lawama kwa watu. Huenda walichangia kuanguka kwako lakini hiyo haiwezi kukuzuia kupata unachotaka.Badilisha mawazo na akili yako na kufanya kile kilicho sahihi. Hakika utafanikiwa. 

Je, ni kitu gani kinakuzuia kuendana na mabadiliko? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 
Imeandaliwa na Lackius Robert 

Wednesday, March 08, 2023

Ni kidogo lakini kinampa faraja

Kila kuna kitu kinampa nguvu kubwa hasa pale anapofanyiwa kitu kizuri. Iwe ni pesa amepewa au hamasa amepata. Kutokana na faraja baada ya kupitia hali fulani nzuri au ngumu. 

Ninapoona sentensi hii napata faraja sana "With people, little things are the big things" ikiwa ina maana ya vitu vidogo, kwa watu vina nguvu sana. 

Ila umfanye mtu ajisikie vizuri huna haja ya kumpa zawadi ya gari, pesa nyingi au kumpatia nyumba. Au iwe na elimu ya juu. Ni kupitia vitu vidogo unavyomfanyia ndivyo humfanya mtu ajisikie vizuri. 

Huenda unajiuliza ufanye vitu gani ili umfanye mtu ajisikie vizuri. Jibu hili hapa. 

Unahitaji kutoa kitu kidogo kinachotoka moyoni mwako. Mfano mtu anaumwa ukaenda kumjulia hali anafurahi. Unamtumia ujumbe au unampigia simu ya kumpa pole. Unamtembelea, huna kitu lakini uwepo wako unampa nguvu kubwa sana. 

Mama amejifungua, umeenda kumjulia hali na zawadi kidogo kwa mtoto. Ni faraja tosha kwa mama mzazi. Sio mpaka uwe na pesa nyingi au ndo uende kumuona. Ujio wako unamfanya ajisikie vizuri. 

Mtu kafiwa na mpendwa wake sio mpaka uwe na vitu vingi kwenda kumfariji au una kiasi kingi  cha pesa nenda. Nenda na hicho kitu kidogo. Kaa naye mfariji mpe pole inamfanya ajisikie vizuri. 

Kwa bahati mbaya walio wengi wetu wanachofanya ni kusubiri wawe na vitu vingi. Kama ni pesa ziwepo nyingi. Kama ni mali au vitu awe na vitu vingi kama vyakula au vitu vingine. 

Ukweli ni kuwa, chochote  kidogo ulichonacho na ukakitoa kwa moyo wako wote kinamfanya ajisikie vizuri. 

Unachotakiwa ni kufanya kile kinachowezekana kwako. Usimpe mtu ukabaki na kinyogo moyoni. Toa kidogo, lakini moyoni ufurahie au ubaki na amani moyoni. 

Hii ndio siri kubwa ya kumfanya mtu ajisikie vizuri. Toa kitu ata kama ni kidogo, ila ukiwa na kitu kikubwa usiache kutoa kikubwa kisa umeambiwa toa kidogo. 

Je, wewe uliwahi kufanyiwa kitu kipi kikakufurahia? 
Bonga nasi hapa hapa 0767702659. 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#37mwangaza2023

Tuesday, March 07, 2023

Hiki ndicho huvunja uaminifu

Ni matumaini yangu kuwa umewahi kusikia watu wakisema fulani kanichomesha mahidi au kaniacha njia panda na maneno mengine. 

Kanipa ahadi hafu kashindwa kuitimiza. Ni hali ambayo inamfanya mtu anakasirika sana. Na mwanzo mpya wa kutopokea simu ya mtu au kukata mawasiliano. 

Huenda imewahi kukutokea au haijawahi kukutokea. Ila ukweli ninaotaka uujue leo ni kuwa: hakuna kitu kinavunja uaminifu kwa mtu kama kutotimiza ahadi. 

Kuweka ahadi ni rahisi ila kazi ipo kwenye kuitimiza. Unapoweka ahadi na mtu, iwe ya pesa au zawadi, jua kuna umakini unautengeneza kwa mtu. 

Kama ni pesa ahadi yako inamfanya aweke mipango juu ya pesa hiyo. Inapotokea hujaweza kutumiza ahadi hiyo lazima mgombane. 

Kuna kitu kinapungua ndani yake ambacho ni uaminifu. Namna ambavyo alikuwa ana imani juu yako anapunguza. 

Ninaposema ahadi sio tu kwenye pesa ata maeneo mengine. Wewe kiongozi umeahidi kutekeleza vitu fulani ndani ya uongozi wako. Muda Miaka mitano inapoisha hujatekeleza. Jua kuna kitu unakipunguza kwa watu wako ambacho ni uaminifu. 

Unahitaji nini ili kutimiza ahadi? Kitu unachopaswa kujua ni kwamba. Sio usome masomo ya juu au usome vitabu 100. Unachohitaji ni uwezo wa kufikiri kilichosahihi kwa wakati sahihi. Usitoe ahadi ukiwa na FURAHA sana au UMEKASIRIKA sana. Toa ahadi ukiwa katika hali yako ya kawaida. 

Kingine, toa ahadi iliyo ndani ya uwezo wako. Epuka kutoa ahadi kwa sifa. Upo mbele za watu au kwenye harusi. Unataka watu wakuone baba la bab au mama la mama itagharimu. 

Weka ahadi iliyo ndani ya uwezo wako. Hii itakusaidia kuitimiza bila kuwa na wasiwasi. Watu wengi huweka ahadi ili wasifiwe inapofika kwenye kuitekeleza ndipo shida huanzia.

Ahadi haipaswi kuwa ile ya kukufanya ukose amani. Inapaswa kukupa hamasa kutafuta zaidi. Weka akilini kuwa, kinachovunja uaminifu ni ahadi hewa. Take care uutunze na kuulinda uaminifu. 

Je, ahadi ipi uliahidi na hukutimiza? 
Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#36mwangaza2023

Monday, March 06, 2023

Uwezo wako wa ushawishi umefichwa huku

Kila mtu anao uwezo ndani yake. Uwezo kwa kumshawishi mtu kuchukua hatua. Katika hili, wapo wanaopata uwezo huu kupitia nafasi zao za uongozi au shuleni. Huku wengine wakiupata kutokana na uzoefu katika kufanya vitu tofauti. 

Ipo njia pekee inayoweza kutumiwa na wote, bila kujali elimu, jinsia wala dini. Na njia hii ni kuwa na shauku kubwa ndani yako. Namna ambavyo unaongea na mtu yeyote kuna kitu anakiona ndani yako. Iwe upole, utii, utukutu au utulivu. 

Ninaposema kuwa na shauku kubwa maana yake ni kwamba; namna unavyoongea na mtu unamfanya awe na umakini kwa sababu kile unachoongea unamaanisha. 

Mtu mwenye shauku anakubaliwa kwa watu wengi. Ipo hivi, tupo kwenye dunia yenye changamoto kila uchao. Watu wengi wanahitaji kupata faraja kutoka kwako. Mfanye kila unayekutana naye afurahi. Na hii itatokana na shauku kubwa iliyo ndani yako. 

Mtu mwenye shauku haogopi, anakuwa na hamasa wakati wote. Anakuwa na uso wa furaha. Sauti anayoitamka inakuwa inatoka vizuri na kusikika tofauti na asiye na shauku. 

Hii ndiyo nguvu kubwa iliyo ndani yako. Mwenye shauku kubwa ya kufanya hakatishwi tamaa na hali anazokutana nazo wala changamoto. Anakuwa na imani kubwa ndani yake. Anapenda wale wanaokutana naye wafurahi zaidi. 

Mmoja kati ya watu waliokuwa na shauku kubwa katika utendaji wao alikuwa Mery Teresa(Mother Teresa) mwanzilishi wa "Mission Of Charity" . Alisifika kuwa na shauku kubwa kuwasaidia watu wanaotoka katika familia masikini. Hii ilifanya dunia itambue mchango wake. 

Haikuishia hapo alipewa tuzo ya Nobel kwa usisitizaji wa upendo kwa watu wanaotoka katika familia za chini. Alikuwa mtetezi wa haki zao. Alipofaliki kanisa katoriki waliamua kuenzi mchango wake kwa kumuita mtakatifu ndipo jina la Mother Tereza likapatikana. 

Moja kati ya misemo yake ilikuwa "The fruit of silence is PRAYER. The fruit of prayer is FAITH. The fruit of faith is LOVE. The fruit of love is SERVICE. The fruit of service is PEACE". Ikiwa na maana, "matunda ya ukimya ni maombi. Matunda ya maombi ni imani. Matunda ya imani ni upendo. Matunda ya upendo ni huduma. Matunda ya huduma ni amani". 

Ukiwa na shauku kubwa ya kufanya vema kitu unachokitaka dunia itaona na watathamini mchango wako. Shauku ni ile nia ya kufanya kitu iliyo ndani yako. Msemo mwingine aliowahi kusema Mother Tereza ni "ishi kama mnyama kufa kama malaika". Akimaanisha fanya kazi yako kama mnyama maana mnyama huwa anasukumwa anapigwa ili kazi fulani zikamilike na huwa hachoki. 

Uwezo wake wa ndani ulidhihirishwa na shauku kubwa. Ile nia na upendo aliokuwa nao kuwasaidia watu masikini. Mchango wake utaenziwa daima na milele. 

Huwezi kuwa kama Mother Teresa ila kupitia yeye kipo kitu unaweza kufanya. Ionyeshe dunia shauku iliyo ndani yako na wafanye walio karibu yako kufurahia uwepo wako. Na mungu atakubariki. 

Je, uwezo wako unafichwa katika kitu kipi? 
Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#35mwangaza2023

Sunday, March 05, 2023

Maono na uwezekano

Maono ni ile picha inayojengeka ndani ya mtu juu ya mambo fulani ayatarajiayo au yatarajiwayo kutokea katika uhalisia. 

Maono haya mara nyingi hufananishwa na picha ya hitaji la mtu analotamani litimie. Mithali 29:18 inasema,
“Pasipo maono, watu huacha kujizuia; bali ana heri mtu
yule aishikaye sheria”. 

Kwa maana nyingine ni kuwa, huwezi kufanikiwa katika maisha yako kama huna maono ya kile
unachotaka kupata katika maisha yako. 

Tofauti kubwa iliiyopo kati ya watu waliofanikiwa na ambao hawajafanikiwa ipo kwenye maono. 

Yaani, ile picha kubwa iliyo ndani mwao kuonyesha kule wanakotaka kwenda. Maono husaidia sana mtu kuweka nguvu kubwa ya kuzingatia kitu anachofanya. 

Lengo lake kuu ni kuhakikisha hatoki kwenye uelekeo wake. Watu wenye mafanikio makubwa ni wale wenye maono makubwa na walio tayari kuhakikisha wanazingatia maono yao. 

Ili na wewe uweze kuwa mtu mwenye uwezo mkubwa wa kuzingatia, lazima uhakikishe unayaishi maono yako.

 William Blake aliwahi kusema, “What is now proved was once only imagined.” Ikiwa na maana kama kitu kimepitishwa au kuhakikiwa basi kiliwahi kuwazwa. 

Hapo unaweza kuona kwamba hakuna kitu kinachokuja bila kufikiriwa au kuwazwa. Hivyo, na wewe unapaswa kuwa na maono makubwa. 

Angalia kitu unachofanya. Kisha angalia kwa miaka minne unataka uwe wapi? Hapo ndipo utaanza kutengeneza picha kubwa kwako. Hayo ndiyo maono unayotakiwa kuwa nayo. Unapokuwa umeweka maono unapaswa kujitoa kweli kweli. 

Angalia aliyekuwa Rais wa Afrika ya Kusini Mzee Nelson Mandela. Akafungwa miaka 27 gerezani. Ile picha aliyokuwa nayo hakuiacha aliisimamia vema. Hadi leo anakumbukwa kwa maono makubwa aliyokuwa nayo. 

Wewe huwezi kuwa Mzee Mandela ila kuna kitu unaweza kufanya kupitia yale uliyojifunza kutoka kwake. Ijenge picha ndani yako ishi nayo uwapo katika utendaji wako, kisha ona uwezekano ndani yake. 

Je, maono yako unayaonaje? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#34mwangaza2023

Saturday, March 04, 2023

Hii ndiyo sababu inayofanya usahau ulichojifunza

Mara ngapi umekuwa unajifunza vitu vingi na kutofanyia kazi hata kimoja? 

Unakumbuka ile siku uliyomaliza kusoma kitabu fulani? Ule mzuka uliotoka nao ukasema nitaenda kufanyia kazi kile ulichojifunza. Ila baada ya siku kadhaa kupita hakuna kilichofanyika. 

Au ulipotoka kwenye semina ya biashara, uongozi, mahusiano au ndoa. Uliwahakikishia watu kuwa unaenda kufanya mabadiliko makubwa sio tu katika kazi zako bali katika maisha yako. 

Kila walipokuuliza uliwaambia umejifunza mambo mengi sana, kiasi kwamba unaenda kufanya maajabu makubwa. Mwezi mmoja mbele hamna kilichofanyika. Umesahau kila kitu. Unataka kujua tatizo ni nini? 

Ipo hivi "To know and not to do, is really not to know. To learn and not to do is not to learn". Kwa lugha nyepesi; kujua kitu na kutokifanya ni sawa na kutokijua. Kujifunza kitu na kutokifanyia kazi ni sawa na kutojifunza. 

Huu ndio ukweli. Unaweza kujifunza vitu vingi lakini ukachagua vile vichache vya kufanyia kazi. Mfano unaposoma kitabu usijipe presha et hadi ufanyie kila kitu. Chagua vitu vichache vya kufanyia kazi. 

Umehudhuria semina, umejifunza mengi. Huwezi kuyafanyia kazi yote chagua machache ya msingi. Umejifunza kuwa, ili uweze kuwa mwekezaji lazima utunze asilimia 30 ya kipato chako, asilimia 10 ya zaka au kumshukuru Mungu. Asilimia 10 msaada au asilimia 50 ya matumizi kwa mfano. Huwezi kuanza vyote kwa pamoja. 

Anza kidogo kidogo na kitu kimoja. Ili baadaye uanze kuzoea. Ila usipofanyia kazi vitu vyote. Jua ni sawa na kutojifunza. Utaelewa zaidi baada ya kuanza kufanyia kazi kitu. 

Mmejifunza biashara. Ili upate ufahamu mzuri wa biashara, fungua biashara. Hapo ndipo utaanza kuona namna gani mambo yanavyoenda na hapo ndipo utapima ubora na uelewa wako, kuhusu mliyojifunza. 

Kila siku, jifunze kitu na ujenge utamaduni wa kufanyia kazi machache uliyojifunza. Itakusaidia kwa kiasi kikubwa kuelewa na kukumbuka zaidi. Ndiyo maana unasahau kile ulichojifunza kwa sababu hufanyii kazi kitu hicho.

Je, ni nini kinakukwamisha kufanyia kazi uliyojifunza? 

Bonga nasi 0767702659 
Lackius Robert 
#33mwangaza2023

Friday, March 03, 2023

Tushirikiane sisi ni wamoja

Nilipata hamasa zaidi niliposoma hadithi inayosema kuwa:

"Kwenye Shule moja kulikuwa na kundi la wanafunzi watukutu ambao walikuwa wakionea wanafunzi wenzao. Wanafunzi hao walikuwa wakikuta mwanafunzi mwingine wanamlazimisha achague wa kupigana naye na akikataa wanampiga wote.

Siku moja kundi hili walikutana na mwanafunzi mmoja aliyeonekana kuwa mnyonge sana. Wakamwambia achague wa kupigana naye. Yule mwanafunzi akachora mstari na kusema yule ambaye anajiona ndio mbabe kuliko wote avuke huu mstari. Yule ambaye ndio alikuwa mbabe alivuka mstari ule na alipofika upande wa pili yule mwanafunzi mnyonge alimwambia sasa tupo upande mmoja, tuungane kupambana na hao wengine. Yule mbabe akakubali wakaliamsha kuwapiga wengine".

Unaweza kuona ni usaliti lakini sio kweli huyu mnyonge alimwambia neno la msingi. Huenda mtoto mbabe hakuwahi kulisikia. Maisha yeke yote aliishi kupigana na kushindana. Lakini alipoambiwa "tupo upande mmoja, hivyo tuungane pamoja". Aliona kuna jambo la msingi.

Hata maisha yetu ndivyo yalivyo. Mnapokuwa upande mmoja mnapaswa kuwa wamoja. Kushirikiana, kushauriana na kushirikishana katika masuala mbalimbali ya maendeleo.Bila kusahau watu wote wanaokuzunguka. Hao mpo nao upande mmoja. Ni vema kusaidiana na kushirikishana. 

Tatizo ni kwamba wengi wetu hatuelewi hii dhana ya umoja. Ndio maana tumekuwa tunashindana lakini hatufiki mbali.

Mfano. Kama wanandoa wangejua kwamba wapo upande mmoja, wa kutaka maisha yao wote kuwa bora basi matatizo mengi sana ya ndoa yasingekuwepo na ndoa zingedumu. Lakini baadhi ya familia, unakuta mme anashindana na mke wake. Wakati mwingine mke anamuibia mali mme wake. Inashangaza sana.

Mwajiri na mwajiriwa hawa wote wapo upande mmoja. Kila mmoja yupo kunufaisha kazi yao na maisha yao kwa ujumla. Lakini mambo ni tofauti huyu anamkwaza na kumkandamiza mwenzake mara anamuibia. Vitu vya kushangaza vinafanyika.

Nashangaa kwanini  tunafikiri kwamba tuko pande tofauti na hivyo kuishia kushindana, mashindano ambayo hayamfaidishi hata mmoja wetu. Mke na mme kushindana, kuibiana. Mtu na mdogo wake kunyanyasana, kutesana na kuibiana. Inashangaza sana.

Wakati ndio huu. Tushirikiane sisi ni wamoja. Tuache ushindani. Baba na mama jenga familia bora. Mwajiri na mwajiriwa ikuze taasisi yenu kupitia umoja. Hakika mtafanikiwa.

Je, nini kinazuia maendeleo yako?

Bonga nasi 0767702659
Imeandaliwa na Lackius Robert
#33mwangaza2023

Thursday, March 02, 2023

Jifunze Ushirikishe

Ukweli ni kuwa kila mmoja wetu kipo kitu anakijua zaidi wengine. Huenda ni upande wa hesabu, lugha, fedha, uongozi, mahusiano au biashara. 

Kila wakati umekuwa mstari wa mbele kujifunza vitu vipya. Lakini cha kushangaza kuna baadhi ya vitu umekuwa ukivisahau. Hali inayokufanya kurudia kuvisoma tena ili vikae. 

Hali hii ya kuwa unasahau kuna wakati imekuwa ikikunyima furaha. Kwa sababu muda ambao ungefanya kitu kingine unautumia tena kupitia. 

Umekuwa unajiuliza namna ipi nzuri kujenga kumbukumbu ya muda mrefu. Njia hii hapa "jifunze shirikisha". 

Ipo hivi "you learn best when you teach another" kwa lugha nyepesi. Unajifunza kuwa bora kupitia kufundisha wengine. Hii ndiyo siri ninayokupa leo. 

Unasoma masuala ya ndoa. Unasoma makala na vitabu vya ujasiriamali, sanaa, biashara au uongozi. Tafuta sehemu au watu wa kushirikisha maarifa yako. 

Inaweza kuwa katika mitandao ya kijamii kama Facebook, Whatsapp, linked au telegram. Au ukaamua kuandika kitabu au jarida, linaloelezea masuala mbalimbali unayojua. 

Uzuri wa kushirikisha ni kwamba unapata uelewa zaidi. Tunasema unachomfundisha mtu kinanasa haraka akilini kuliko kile usichoshirikisha. 

Jifanyie tathmini. Hata kama ni vitu vya kawaida kama kumfundisha mtu kutumia simu, kupika chakula fulani. Namna unavyokumbula hatua zote. Na pengine unahisi kama yule uliyekuwa unamfundisha upo unamuona mbele yako. 

Wenye uwezo mzuri wa kutunza kumbukumbu hawajashushwa kama ulivyokuwa unadhania. Walichukua wajibu kujifunza na kushirikisha yale wanayojua. 

Wakati ndio huu. Ifanye dunia ijue kile kilichomo ndani yako. Ili baadaye uwe na uwezo mkubwa kuwa na kumbukumbu nzuri. 

Je, nini kilikuwa kinakukwamisha kuweka kumbukumbu zako? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#32mwangaza2023

Wednesday, March 01, 2023

Fanya kinachowezekana

Ni mara nyingi tumekuwa tunaacha kufanya baadhi ya vitu kwa kujipa moyo kuwa ni vigumu kufanyika. Unakuta mtu anafanya kitu kwa muda mchache anaacha kisa kuna ugumu anauona au kukutana nao. 

Lakini ukweli ndio huu kwamba vitu vingi, ili vikamilike kuna juhudi nyingi zinapaswa kutumika. Juhudi hizi zinapaswa kuwa endelevu zaidi ya kawaida. Sasa wengi wetu baada ya kuona juhudi nyingi tunazoweka bila kupata matokeo huwa tunakata tamaa. 

Hali inayofanya tushindwe kabisa kufanya vitu. Na pengine kuamua kufanya vitu vingine vipya zaidi tukihisi vitu vya kwanza havijafanya kazi. Leo ipo njia pekee nimekuletea nakushauri uifanyie kazi.  Sio njia ambayo ni nyepesi kufanya ila ukiifanya kuna kitu kinaweza kuongezeka au ufanisi fulani katika kazi zako. Njia hii ni hii hapa. 

Fanya kinachowezekana. 

Hii ni njia na msemo unaoweza kuutumia kila siku katika maisha yako na utendaji wako. Kabla hujaacha kitu na kuanza kingine hakikisha kitu kimefanyika au jambo limefanyika. Umepanga kitu kabla hujakifanya unaachia njiani nakushauri kuitumia njia hii. Wewe fanya kile kinachowezekana. 

Ni binti unahitaji kuzungumza naye kabla hujaacha fanya kitu. Usijipe majibu. 
Kwa taarifa yako hakuna vitu au biashara inayoanza ikiwa kubwa wala mafanikio yanayoanzia juu. Vyote vinaanzia katika hatua za awali. Ikiwa na maana ya wahusika kufanya kile kinachowezekana. 

Unataka kufungua duka. Fungua kisha unanze kuuza kadri utakavyoweza. Fanya kinachowezekana kufanyika. Usishindane na watu. Wewe fanya kilicho ndani ya uwezo wako wote. Hii itakusaidia kuona wapi panahitaji maboresho au kufanyiwa kazi zaidi. 

Uzuri wa kufanya kinachowezekana ni kwamba unapata nguvu ya kuendelea zaidi. 

Kila mara kabla hujaacha kitu jiulize je, nimefanya? 
Kisha rudi kwenye msingi wa kufanya kinachowezekana kufanyika. Wasiliana nasi 0767702659.

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#32mwangaza2023

Tuesday, February 28, 2023

Hiki ndicho kinachotupoteza

Katika zama tulizomo kuna vitu ambavyo tumevipa nguvu na vimefanya tukose usingizi. Ila kuna kitu bado tunakipuuzia. 

Huenda umekuwa unajiuliza kwanini ajali nyingi zinazidi kutokea, na kwa nini haziishi licha ya uwepo wa askari usalama barabarani sehemu nyingi? Na sheria kali. 

Jibu ni moja tunakosa umakini. 

Kwanini siku hizi majibu ya mitihani kwa watoto wetu hayaridhishi kwa kiwango cha juu? Jibu ni moja tu hakuna umakini. 

Kwa nini biashara nyingi zinakosa kuwa na mauzo mazuri, licha ya kuwepo mwa mzigo wa maana. Jibu ni moja umakini. 

Umakini ni suala ambalo wengi wetu tumelipiga kisogo. Tunaweka jitihada kujifunza tena kwa kulipia, wakati mwingine kununua baadhi ya vitu ili tusonge mbele kwa kukosa umakini tunashindwa kuvifanikisha. 

Siku hizi suala la kukuta mtu anaongea na simu wakati akiwazaa kitu kingine ni la kawaida. Yaani anongea na simu ya muhimu huku yeye akiwa na kitu kingine kisicho muhimu anachokikazania. Ndio maana mwisho wa mazungumzo ukimuuliza mlichozungumza anashangaa. Ndio uhalisia tulionao. 

Tumepoteza umakini kwa kiwango cha juu. Tunakoelekea sio kuzuri. Faini zimewekwa za kutosha mfano dereva hupaswi kuendesha mwendo fulani huwapo sehemu fulani. Kwani wanasikia basi. Tunaambiwa kuovertake gari ni hatari. Lakini ajali ngapi hutokea? Ni kukosa umakini. 

Hata kwenye familia janga lipo kubwa. Mtu anapika chakula lakini akili yake ipo kwenye TV ili aangalie tamthiliya fulani. Matokeo yake chakula kinaungua. Mume akija vurugu zinaanza. 

Walio kwenye mahusiano ya kawaida pia. Mtu yupo na mwezi wake lakini mawazo yake yapo mahali pengine. Unaweza kushangaa lakini ndio ukweli. Au unaweza kuwa unaongea na mtu anakutazama lakini ukimuuliza kitu anashtuka au anashangaa sana. Ni kwa sababu hajaweka umakini kwako. 

Wengi tunaruhusu vivuli vyetu kuwa mbele za watu. Upo na mtu karibu lakini mawazo na kila kitu havipo hapo. Hiyo hali sio sawa. Wakati ni sasa. Weka umakini kwa kitu unachofanya ili ukifanye kwa uzuri zaidi. 

Weka moyo wako na akili zako zote kwa kitu unachofanya. Hakika utakifanikisha. 

Je, ni nini kinakufanya ukose umakini? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#31mwangaza2023

Monday, February 27, 2023

Juhudi na uvumilivu

Msemo wa mvumilivu hula mbivu unayo maana kubwa katika maisha ya mwanamafanikio yeyote. Ikiwa huna uvumilivu mambo mengi hutakubali yakupite. Lakini huo ndio ukweli. 

Kuna wakati utaweka juhudi kubwa katika kitu fulani lakini huoni matokeo. Sio kwamba unakosea au haupo sawa. Bali muda haujafika. Hakuna aliyefanikiwa katika jaribio la kwanza. Wote walifanya majaribio mengi zaidi yaliyopelekea baadaye kufanikiwa. 

Mafanikio yao hayakutokana na juhudi tu bali na uvumilivu mkubwa. Chukulia mtoto mdogo anapozaliwa. Inachukua muda mrefu kuona ameanza kutembea kuongea na kukimbia. Lakini kila mara kuna kitu anakuwa anafanya. 

Kadiri muda unavyozidi kwenda ndivyo anavyokuwa anafanikiwa eneo moja. Hawezi kuanza kukimbia moja kwa moja anaanza na kutambaa baadaye kusimama. Kisha kukimbia. Sio zoezi la siku moja wengine inachukua miaka miwili. Katika nyakati hizo mtoto hachoki kuonyesha jitihada kubwa na uvumilivu pale aangukapo. Ni katika kuvumilia ndipo juhudi zetu huzaa matunda. 

Kuna wakati unafanya kitu ukiwa na matarajio makubwa lakini hupati matokeo unayoyataka. Ila kwa kuwa una uvumilivu ndani yako unazidi kufanya. 

Muda unapofika. Kila kitu kinakuwa sawa. Ndiyo maana ya mvumilivu hula mbivu. Changamoto unazopata au ukinzani unaokutana nao unakujenga zaidi kuwa imara. 
Mchanganyiko wa nyakati ngumu huwa haudumu zaidi. Unachohitaji ni kuwa na uvumilivu huku ukiendelea kuonyesha jitihada zako. 

Jifunze kuona uwezekano katika nyakati ngumu. Hiyo itakusaidia kuongeza jitihada maradufu. Hakuna kinachoshindikana kwenye uvumilivu na jitihada. Mara zote kuwa mtu wa kufanya. Wewe fanya, hata kama ni wakati mgumu jaribu kufanya. Mambo yatajipa. 

Je, ni wakati upi mgumu hutousahahu? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#30mwangaza2023

Sunday, February 26, 2023

Jipongeze mwenyewe

Wakati nasoma sekondari alikuwepo mwalimu mmoja aliyekuwa anapenda kutumia msemo wa "ikiwa watu hawakusifii au kukupongeza kwa kizuri unachofanya unapaswa kujipongeza mwenyewe".

Ni kweli alikuwa anafundisha vizuri katika masomo ya sayansi hasa kemia na fizikia. Wanafunzi wengi waliokuwa wanafaulu  walitoka kwenye masomo yake. 

Wakati anatufundisha alikuwa anapendelea kuutumia msemo tajwa hapo juu. Akimaanisha licha ya kufanya vema shuleni kwa kufundisha kwa moyo wote lakini hakuwa anapata pongezi sahihi. Akawa anatwambia badala ya kukatishwa tamaa na hilo au kusubiri pongezi. Wewe jipongeze mwenyewe. Hii itakupa hamasa kubwa kiutendaji. Alikuwa anajipongeza mwenyewe. 

Ni ukweli usiopingika kuwa zama tulizomo zimekosa subira. Vitu vingi vinawekwa wazi. Hakuna siri tena. Wengi wetu tunaweka picha kwenye mitandao tukisubiri comments na likes kulingana na mahudhui tuliyoweka. Zinapokosa tunaumia sana. Hasa tunapoona wenzetu wanazipata kwa kiwango kikubwa tunaumia zaidi. 

Pengine huchangia kukata tamaa katika baadhi ya kazi zetu. Huku baadhi tukiamini hawatuthamini au kujali kazi zetu. 

Katika hali kama hizi tunaumia sana. Ila ndio ukweli kuwa; dunia imekosa subira. Haipo tayari kukupa pongezi inahitaji ukae au urudi hatua chache nyuma ya ulipo. 

Turudi kwenye msemo wa mwalimu wangu. Aliamua kujipongeza mwenyewe. Hii inaitwa "self recognition" unajipongeza mwenyewe. Lengo kuu ni usichoke wala kukata tamaa au kuacha unachofanya. 

Chukulia mti kama mwembe au mpera. Haujawahi kupongezwa kwa kazi yake badala yake unapigwa mawe na kukatwa. Lakini bado haujawahi kuacha kutoa matunda kila msimu unapofika. 

Hata wewe unahitaji kuweka nguvu katika kazi zako. Waseme wasiseme endelea kuchapa kazi. Jisifu na jipongeze uwezavyo. Itakusaidia kwa kiasi kikubwa kuongeza hamasa katika utendaji wako. 

Nyakati za furaha, furahia. Nyakati ngumu au uangukapo piga moyo konde endelea na kazi. Utajisogezea baraka na nguvu kubwa. 

Je, wewe unasubiri kupongezwa? 
Bonga nasi hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#29mwangaza2023

Saturday, February 25, 2023

Furahi zaidi leo

Tunaishi mara moja. Hili endelea kulikumbuka katika utendaji wako wa kila siku. Huenda linakuja na kutoka katika maisha yako. 

Kwanini ninasema, furahia zaidi leo? Ni kwa sababu mafanikio na furaha ni vitu vinavyoenda pamoja. Ikiwa huna furaha hutapata mood ya kufanya kazi. Na bila mood ya kufanya kazi basi hamna maendeleo yoyote. 

Wengi wetu tunasema hatuna furaha kwa sababu hatuna pesa. Tunasahau hili kuwa; kama furaha yako ni pale utakapopata pesa. Basi tambua furaha yako haitapatikana daima. Maana pesa ni namba hazina mwisho.

Ukiwa na laki moja utahitaji milioni moja. Ukiwa na milioni moja utatamani milioni kumi. Ukiwa na milioni kumi utataka ishirini au therathini. Kadri utakavyozidi kupata pesa zaidi ndivyo utazidi kuhitaji pesa zaidi. 

Ni nini kifanyike? 
Kuwa na mtazamo kuwa pesa yotote uliyonayo ni zao lako na unapaswa kuifurahia. Hii ni kwa sababu kupitia kuifurahia ndipo utapata kubwa zaidi. Maana ukiwa na furaha utaweza kupata nguvu za kutafuta zaidi. 

Usiseme sina pesa nyingi. Hivyo, siwezi kutoa msaada kwa watu. Usubiri upate pesa zaidi. Hilo halitawezekana. Pesa ni namba na namba hazina mwisho. Hivyo, kuitafuta kwako furaha hakutakuwa na mwisho. 

Timiza wajibu wako kufanya kazi yako kwa ubora hata kama malipo ni kidogo. Usiache kufanya endelea kusonga mbele. Iwe wakati wa jua au mvua wewe fanya tu. Matokeo mazuri huwa yanaanzia kwako kwa kufurahia kazi yako. 

Hutapata nafasi ya kuishi tena hapa duniani. Nafasi ni moja tu. Ikiisha imeisha. Furahia leo zaidi kisha fanya zaidi

Je, wewe furaha yako iko wapi? 

Bonga nasi hapa hapa 076772659 
Lackius Robert 

#28mwangaza2023

Friday, February 24, 2023

Tunategemeana ili maisha yaende

.            Nikiwa na nazungumza na                             wanafunzi wa shule moja Dsm.

Sio rahisi na haitakuwa rahisi hadi mwisho wa dunia. Kwamba et, kuna mtu anayeweza kusimama mbele ya  watu na kusema; mimi ninaweza kufanya kila kitu ili maisha yaende. Mimi ni jeshi la mtu mmoja ninaweza kila kitu peke yangu. 

Yaani anajitibu, anajiendesha, anajipikia, anajifulia, anajitengenezea bidhaa au mahitahi mengine. Hii sio kweli. Kwa namna moja au nyingine tunategemeana kwa kiasi kikubwa msaada kutoka kwa watu wengine. Sio kifedha tu bali mawazo, nguvu na ushauri wetu. 

Mfano mchungaji hawezi kusimama mbele ya kadamnasi na kusema mimi nayaweza mambo yote peke yangu. Anahitaji waumini. Katika kuendesha kanisa ikiwemo sadaka na utawala. 

Mfanya biashara hawezi kuvimba mbele ya watu kuwa, anapata pesa kivyake au kwa juhudi zake. Lazima awategemee wateja kununua bidhaa zake. Bila wateja hakuna manunuzi. Unaweza kuwa na bidhaa zote. Wateja wasipokuja, huwezi kuongeza vingine. Ndio maana upo msemo wa mteja ni mfalme. Kupitia manunuzi ndipo biashara inakua.

Mwanamme au mwanamke hawezi kujigamba mbele za watu oh mimi ni mimi. Nina watoto wa peke yangu. Hivyo, ninajitosheleza. Kumbuka, huwezi kupata mtoto bila kuwa na mwanamme au mwanamke. Kwa sababu mtoto hashuki kutoka mbinguni au kwenye chai. Lazima jinsia mbili wakutane kimwili(Kufanya tendo la ndoa). Baadaye mtoto apatikane. Tunategemeana kumbuka. 

Mwanasiasa hawezi kusimama au kuzungumza mbele ya vyombo vya habari akijigamba yeye ni yeye anaweza kila kitu. Ni makosa. Anawategemea waliomuweka kwenye kiti ambao ni raia. 

Ninaweza kuandika hadi kesho lakini point ni kwamba tunategemeana. Wakumbuke wahenga, "Umoja ni nguvu, utengano ni udhaifu". Ni dhahiri unamtegemea mtu mwingine kukamilisha umoja huu. 

Shule inahitaji walimu. Walimu wanahitaji wanafunzi. Wanafunzi wanawategemea wazazi. Soma kurudi nyuma. Wazazi wanategemea wanafunzi kuwapeleka shule. Shule inahitaji walimu ambao wanawategemea wazazi. 

Wewe sio jeshi la mtu mmoja. Kuna watu walikufanya kuwa hivi ulivyo kwa sasa. Heshimu, saidia na wajali watu bila ubaguzi wa aina yoyote. Safari yako ya mafanikio sio ya peke yako. Unahitaji watu kuifanikisha. 

Je, unaweza kufanikiwa ukiwa peke yako? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#27mwangaza2023

Thursday, February 23, 2023

Huku ndipo nguvu zako uanzia

Umewahi kumuona Paka katika sehemu zenye taabu. Ikiwa na maana kwenye jua kali, moto mkali au sehemu hatarishi. Jibu ni hapana. Unataka kujua kwa nini? Twende pamoja.

Tupo katika dunia yenye changamoto nyingi zaidi. Kadri muda unavyozidi kwenda mbele ndivyo zinavyozidi kuongezeka. Kuongezeka kwa changamoto hizi kumewafanya baadhi yetu kukosa utulivu.

Hii imewafanya kila mara wapatapo changamoto kukimbilia kwenye mitandao ya kijamii kupost n.k. Nia yao kuu ilikiwa ni kupata msaada juu ya magumu yanayowakabili. Matokeo yake imekuwa tofauti na kufanya mfadhaiko kwao kuzidi kuwa mkubwa.

Wanachoshindwa kujua ni kuwa mitandao ya kijamii haiwezi kutatua kila tatizo. Kwa sababu kule unakutana na watu wengine wenye matatizo. Hivyo, tatizo linazidi kuwa sugu. Na kinachoongeza uzito ni kule kusemwa au kusimangwa ambako mtu hukutana nako kwenye mitandao.

Siku ya leo nimekuja na njia mpya kukusaidia kutatua changamoto hiyo. Ukumbuke hapo juu nimeanza kukuuliza swali kuhusu Paka. Namna anavyopenda starehe na kukataa maisha ya shida. Utamkuta amekaa kwenye kochi ametulia. Amekaa kivulini uvunguni mwa gari. Amekaa sehemu ya upepo safi na tulivu. Lengo kuu ni kuponya majeraha anayokutana nayo katika harakati zake za utafutaji wa chakula.

Kwetu binadamu sehemu inayoenda kuwa baraka kwetu ni sehemu yenye utulivu kwa maana ya faragha. Huko ndiko nguvu zinakotoka. Maana unapata nafasi ya kutafakari kwa kina juu ya hali mbalimbali unazopitia katika maisha yako.

Kuna wakati tunaona kama tuna changamoto lakini unapopata muda wa kutafakari utagundua vitu vingi. Uwezekano wa vitu unaanzia kwenye fikra. Akili yako itakuwa na uwezo mkubwa wa kuwaza vitu na kutafuta suluhu. Una changamoto ya mauzo, ndoa, mahusiano  au kazini. Tafuta eneo tulivu utulie kisha ujitakafari zaidi. Mara zote ikumbuke hii "tenga muda wa kufikiri kwa sababu ndipo kuna chanzo kikubwa cha nguvu zako"

Je, uko tayari kutafuta nguvu hizo? Bonga nasi hapa hapa 0767702659

Lackius Robert

#27mwangaza2023

Wednesday, February 22, 2023

Sikiliza ila fanya kinachofaa...

Ni kawaida yetu binadamu kutoa ushauri au mapendekezo pale inapobidi au tunapoombwa. Katika hili wengi wetu tumekuwa tunatoa mapendekezo au ushauri wa moja kwa moja hata kwa baadhi ya vitu ambavyo hatujawahi kufanya. 

Wakati mwingine hujawahi kufanya biashara fulani. Mtu anapokuomba ushauri kutokana na changamoto anayopitia. Wewe unamwambia haa! kama wateja wachache achana nayo. Fungua nyingine. Tena unamhakikishia inaenda kumlipa zaidi. Cha kushangaza hiyo unayomshauri hujawahi kuifanya unaisikia kwa watu. 

Hii ilimpata rafiki yangu  Japhet japo sio jina lake halisi. Aliomba ushauri kwa rafiki yake. Bahati mbaya rafiki yake alikuwa ni wale wanaotoa ushauri wa moja kwa moja. Tena kwa msisitizo wa hali ya juu. Na hakuwahi kufanya biashara yoyote.

Wakati Japhet alikuwa anafanya biashara ya nguo. Alikuwa anafungua saa nne na kufunga saa kumi. Hivyo, wateja wakawa ni wachache anaowapata kulingana na muda anaofungu na kufunga. 

Baadaye akaona mtu wa muhimu kuomba ushauri ni rafiki yake. Akaenda, wakazungumza. Akajielezea kuwa; biashara yake imedolola hapati faida wateja ni wachache, anapata hasara. 

Rafiki yake, kusiki hivyo. Akamwambia Japhet. Wewe hiyo biashara ya nguo achana nayo. Haiwezi kukulipa. Fanya biashara ya viatu. Hii inalipa sana. Karume pale viatu afu 3,000. Baadaye unauza elfu 10,000 hadi 20,000/= raha na biashara tamu mdomoni. Rafiki yake kamwambia atafute pesa kiasi fulani kwa kuuza nguo zilizopo. Ili baadaye aanze kuuza viatu. Na akamwambia yeye atakuwa mteja wa kwanza kununua viatu. 

Japhet akasahau msemo wa "Usichinje Ng'ombe kwa oda ya maini". Akafanya kama alivyoambiwa. Akaacha biashara ya nguo na kuuza viatu. Akaweka matarajio mengi. Anaenda kupata faida kubwa zaidi ya ile ya awali. Akafanya haraka maamuzi.

Muda mrefu amefungua rafiki yake hajafika kuchukua viatu. Kila akimpigia kumtaka anunue anampiga kalenda. Imekuwa changamoto kubwa zaidi ile ya awali. Pesa alizotumia hata kurudi bado. Wateja wanaokuja mara nyingi ni wale wanaohitaji nguo. Yale aliyotarajia hakuyapata. Akaanza kukata tamaa. 

Pesa alizotumia bado hazijarudi. Mtaji wa kununua nguo hana hadi maumivu. Akaumia sana kufanya maamuzi ya haraka sana. 

Huenda upo kwenye kada nyingine. Biashara nyingine, upo kwenye ndoa. Take care do what is right for you. 

Funzo: 
Kabla hujaenda kuomba ushauri kwa mtu jitafakari kwanza. Mfano Japhet alikuwa anafungua saa nne na kufunga saa kumi. Ni muda mchache sana. Hili lilikuwa tatizo la kwanza.

Unapata changamoto namna ya kuitatua. Nenda kwa mhusika. Ambaye amewahi kuipitia hiyo au ana uzoefu zaidi yako. 

Sikiliza ushauri wa kila mmoja ila fanyia kazi yale unayoona yanafaa kwako. 

Biashara yoyote ile inalipa ukiifanya kwa nguvu zote, upendo na moyo wako wote. 

Je, ni maamuzi gani uliyofanya yakakuangusha? Bonga nasi hapa hapa 0767702659

Imeandaliwa na Lackius Robert. 

#26mwangaza2023

Tuesday, February 21, 2023

Inuka, unayo nafasi

Ni kawaida ya kila anayetembea kuanguka. Au kila anayeweza kusimama. Iwe katika nyakati nzuri au mbaya. Kuanguka kupo tu. 

Shida inakuja unaanguka katika mazingira yapi. Je, unaweza kunyanyuka au huwezi? Na ni nani wa kukusaidia?

Huenda hujaelewa point yangu. Ni kweli, umedhamiria kuacha tabia fulani kitu fulani. Kilichokuwa kinakurudisha nyuma. Hasa pale unapokuwa unakifanya. 

Inaweza kuwa kulewa, kutembea usiku, kuiba, kuwasema vibaya watu, matumizi ya pesa hovyo. Na mengine mengi. 

Umejaribu kila mbinu imeshindikana. Badala ya kusimama umejikuta unaanguka tena. Leo ninao ujumbe mzuri kwa ajili yako. 

Inuka, unayo nafasi. Ruhusu mwili wako kuona uwezekano juu ya tabia unayotamani kuiacha. Maana mwili wako, umekuwa unachangia kukupa sababu kwa kiasi kikubwa. Kila unapotaka kujitoa umekuwa unakupa mapingamizi. Unahisi kuchoka na hatua za mabadiliko. Unaona kama haiwezekani kabisa. 

Ukweli ni kuwa hii hatua unayotaka kuipiga haitakuwa ya siku moja. Inahitaji ufanye maamuzi magumu. Haya yatapelekea wewe kuingia kwenye mchakato sahihi. Kukaa kwako kwenye mchakato kutakuja na majibu tofauti tofauti. 

Mchukulie mtoto mdogo, anapokuwa katika hatua za ukuaji. Kila anapotaka kutambaa au kusimama mwili unagoma. Kinachomsaidia kutoka hapo ni kwamba, anaulazimisha kufanya kile anachotaka kufanya. Inachukua muda lakini baadaye anazoea. 

Wakati ndio huu ile tabia inayokuangusha na kukurudisha nyuma kuiwekea mpango wa kuiacha. Inuka, unayo nafasi. Na ni rahisi sana kuifanikisha. 

Kuanguka ni jambo la kawaida. Kubakia chini ndio mwiko kabisa wa safari yako. Anguka, inuka, simama na usonge mbele. Ipo nafasi kwa ajili yako. 

Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659 

#25mwangaza2023

Monday, February 20, 2023

Usiangaike na maneno yao...

Kwenye maisha, watu wanayo nafasi ya kuamua kulingana na wanavyoona. Iwe ni sahihi au sio sahihi. Wanakuwa wanaamini wanachokisema kwa asilimia mia moja.

Inapotokea wewe ukawapinga inakuwa ngumu kukuelewe. Maana tayari kipo kitu wanakiamini kutoka kwao. Unachotakiwa kuzingatia ni yale unayoona yanafaa.

Ndio maana huwa ninasema mara zote wewe amua upande unaotaka. Maana ukifanya wanasema, usipofanya wanasema na ukiacha watasema pia. Pale unapoona panafaa ingia upande huo. Kisha fanya kinachowezekana kufanyika.

Wanakusema sio kwamba unakosea bali kuna hatua kubwa wanaona unaenda kuipiga. Hiyo, ndio inayowafanya wanakusema. Ukiweka nguvu kuyasikia maneno yao itakuwa ni ngumu kuendelea.

Hata wale walio karibu yako huwezi kuwazuia kusema. Nao watasema kulingana na namna wanavyoona inawafaa.

Wakati mwingine hata ukifa bado watasema kuwa fulani alikuwa hivi ama vile. Wajibu wako kama mtu unayetaka kufanikiwa kuweka nguvu kwenye kazi zako.

Huenda unajiuliza maswali, ufanye nini sasa?
Maana ukweli ndiyo huo kuwa, watu lazima watakusema iwe unafanya au hufanyi. Watasema bila kuwa na wasiwasi wowote.

Nakushauri, usiangaike na maneno ya watu juu yako. Usiangaike weka nguvu kwenye kazi zako. Fuata moyo wako kwa kile unachotaka kufanya. Pia, fuata ushauri huu wa aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza Winston Churchill aliwahi kunukuliwa akisema,“Kwa muda mrefu Sasa nimeacha kuwasikiliza watu, badala yake naangalia kile wanachofanya. Tabia ndiyo ukweli pekee.”

Hutawazuia kusema ila unaweza kujizuia kufanyia kazi yale yasio mazuri kwako.

Imeandaliwa na Lackius Robert
0767702659

#25mwangaza2023

Sunday, February 19, 2023

Hiki ndicho hupoteza nguvu zako

Alikuwepo bwana mmoja tumuite Chris japo sio jina lake halisi. Alikuwa fundi mzuri katika masuala ya kutengeneza magari. Chris alikuwa analalamika sana kuhusu kazi kuwa kubwa na haoni matokeo. Anasema, wakati anafanya kazi moja, inakuja nyingine nzuri zaidi anaikimbilia. Mwisho wa siku anajikuta amechoka sana kwa kufanya mambo mengi. Ila akijaribu kupima uzito wake anaona nguvu aliyotumia ni kubwa kuliko matokeo aliyopata. 
 
Chris aliona ni vema kumtafuta mtaalamu wa msuala na maendeleo binafsi(Personal Development Issues) ili aone kama anaweza kupata masaada. Siku ilifika mtaalamu akaonana naye. Akajielezea namna anavyotaka asaidiwe. Mtaalamu alimsikia vizuri akamwambia sentensi moja. Naomba ukimaliza kazi zako leo, niandikie vitu vitano na vikiwa sita sio mbaya  unavyoenda kufanya kesho. 
 
Chris akamuangalia mtaalam na kumuuliza, ina maana kukuita kwangu kote hapa na malipo ninayokupa hiki ndo umeona kinaweza kunisaidia? Mtaalamu akamwambia, naomba usinipe pesa yako. Ila hivi vitu vitano nilivyokwambia wewe nitumie. Kisha endelea kufanya hivyo kwa kipindi cha mwezi mmoja. Utaniambia nafaa kulipwa au kukulipa? 

 Chris  alilalamika sana kwa kutosikia neno la hamasa na pole kutoka kwa mtaalam. Kwa mbinde sana akakubali kisha kufanya kama alivyoambiwa. Akilini mwake alifanya kama kumkomoa mtaalamu. Kweli vitu vitano au sita tu ndo nifanya kila siku? Mh! Hapa nimekula kamongo. Haya! Ngoja nifanye nione. 
 
Kesho yake akamtumia orodha ya vitu hivyo. Na siku hiyo ya kwanza akafanikisha kufanya vitu vinne pekee. Siku iliyofuataalifanikisha vitu vitatu. Baada ya wiki moja Chris akaangalia kwenye orodha yake. Akagundua bado hata hivyo sita hajavifanya katika kiwango kizuri na kila akipanga havimalizi. 

Akaamua kuweka nguvu kwenye kuzingatia orodha yake. Siku inapoisha anapitia kuona kama alivyokamilisha ni kweli au la. Baada ya mwezi mmoja kuisha aligundua vitu vingi sana. Kwanza alianza kuiona kazi yake kama inampa matumaini kifedha na mambo ya muhimu angalau yalikuwa yananyika. Hii ni kwa sababu alikuwa anaenda na namba zake. 
 
Baada ya hapo aliomba kuonana na mtaalam kwa ajili ya kumpatia mrejesho na ushauri mwingine. Mtaalamu alikubali ombi lake na akaja tena ofisini kwake Chris Mazungumzo yalianza huku Robby akianza kuomba samahani wa maneno makali aliyotamka siku ile. Na akasema, mwanzoni nilichukulia kama kitu cha hovyo kisicho na maana lakini nilivyoanza kukufanya niliona ugumu na umuhimu wake. 
 
Siku zilivyoenda nikawa ninapata unafuu najikua hata muda wa kupumzika ninaupata. Kitu ambacho hapo awali akikuwepo. Nilikuwa bize asubuhi hadi jioni. Huwezi amini hadi mke wangu kipenzi Mama Joy anashangaa ninaenda mapema nyumbani huku nikiwa sina kazi nyingi za kufanya tofauti na hapo awali. Kwakweli , ninakushukuru sana. Naomba tu nikupe hiki kiasi cha pesa kama shukurani. Umenisaidia pakubwa naomba uwe unafutailia maendeleo yangu nitakulipa kiasi utakachoniambia. Mtaalamu akampongeza Chris na kazi ikaendelea. 
 
Huenda na wewe unapitia hali kama aliyokuwa anaipitia Chris Siku yako inakuwa na vitu vingi ambavyo mwisho wake ukiangalia hamna cha maana kilichofanyika. Inafika mahali unakosa muda wa kukaa na familia yako. Wakati ndio huu. 

Kumbuka,  kuweka orodha ya mambo unayoenda kuyafanya wa siku ni kitu cha muhimu zaidi. Wengi wetu tumezoea kusema vitu vyangu navijua kichwani sikia, "wino uliokauka ni bora kuliko akili" kwa sababu akili inaweza kusahau lakini wino ulioandikwa tayari hauwezi kuondolewa.      
Kuweka orodha ya mambo unayoenda kufanya kwa siku sio zoezi jepesi maana wengi wetu hatuna mazoea. Ni zoezi linalohitaji msukumo na ufuatiliaji wa mara kwa mara. Ikiwa ukifanikisha hili utakuwa na uwezo mkubwa wa kufanya mambo yako yasonge mbele. Siku ya leo unapomaliza kusoma makala hii anza kuweka orodha ya mambo unayoenda kufanya kwa siku yako inayofuata ili yakusaidie zaidi.

Je, wewe siku yako unaianzaje? 
Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#24mwangaza2023

Saturday, February 18, 2023

Umuhimu wa kuwa Orodha ya Vitu vya kufanya(To do list)

Ndugu yangu mpendwa: 
Usiianze siku yako ya bila kuwa na orodha ya majukumu unayokwenda kuyakamilisha kwenye siku hiyo. Majukumu hayo yanapaswa kupangwa kulingana na vipaumbele vyake na hayapaswi kuwa mengi sana. Idadi ya majukumu yawe angalau tano au sita muhimu ya kukamilisha kwa siku ni nzuri ambayo ukiifanyia kazi utakuwa na matokeo mazuri. Ikiwa orodha itakuwa na vitu vingi utaona uvivu kuvikamilisha. Hii ni kwa sababu akili yetu imeumbwa hivyo. Vitu vikiwa vingi huwa inatafuta namna ya kuvikwepa. 
 
Naomba tuelewane katika hili; kwenye uandaaji wa orodha yako usiweke vitu hivi kuoga, kula, kulala hivi vinajulikana. Unaweza kuvifanya ukiwa katiza kazi yoyote ile. Orodha yako iendane na majukumu yako kikazi. Kama unafanya kazi katika ofsi fulani orodha yako ilenge majukumu hayo. Kama unauza duka, unasuka nywele weka ahadi ya kusuka watu wegi zaidi. Kama wewe ni bodaboda weka orodha ya kwenda safari nyingi zaidi. 
 
Ninakuandikia hivi kwa sababu kubwa watu wengi hupoteza muda  kufanya mambo kwa mihemko. Ili  kukabiliana na kila jambo linalokuja mbele yao. Wanakuwa hawana kipaumbele chochote kwenye siku yao, hivyo chochote kinachokuja mbele yao kinakuwa ndiyo kipaumbele kwao. Hali inayopelekea mwisho wa siku kuambulia kitu kidogo. 
 
Kwa mfano unaweza kuwa umepanga kukamilisha yafuatayo;

1. Kujifunza kwa kusoma kitabu kulingana na uhitaji wako, au kuhudhuria kikao 

2. Kuonaana na bosi katika taasisi fulani, kufungua duka au kwenda sehemu kufutilia mzigo.

3. Kuwahudumia na kuwatembelea wateja 5, kuandaa ripoti au kupiga simu ya ufuatiliaji wa malipo.

4. Kufuatilia ahadi ambazo wateja walitoa, bosi au rafiki, kuandaa cheque list ya malipo au quotation kwa ajili ya kampuni fulani kulipia. 

5. Kuweka miadi na wateja wapya viongozi,  marafiki au kutembelea ofisi fulani kwa ajili ya kupata taarifa fulani(visitation).

6. Kufanya mazoezi, kupeleka cheque benki, kufanya matembezi na familia au rafiki. 
 
Orodha hii utaitengeneza kulingana na namna unavyotaka mambo yako yawe ndani ya siku husika. Orodha inakuwa kama mwongozo wako kwa siku. Pia inakupa hamasa kutimiza kile ulichopanga kwa ufanisi wa hali ya juu. Bila kuweka orodha nzuri utajikuta ukifanya mambo mengi yasiyo na tija. Hii ni kwa sababu mambo hayajwahi kupungua. Wakati unafanya hili litajitokeza lingine. Utaona ni muhimu kulifanya ujakaa sawa linaingia jingine mwisho wa siku utajikuta umechoka sana na ukiangalia ulivyofanya havieleweki au kukupa nguvu. 
 
Nakusihi usijifunge au kukosa amani kisa ujatimiza au kukamilisha kila kitu ulichoweka kwenye orodha yako. Wewe zingatia utendaji, kilichofanyika kikakamilika ni bra kisichofanyika. Siku hazilingani leo unaweza usitimize yote uliyoweka kesho ukayatimiza yote. Inapotokea hujatimiza yote usijisikie vibaya. Jipange kesho ingia kwenye utendaji. Lakini hii isiwe sababu ya wewe kuzembea ukijipa moyo nitafanya hata nisipotimiza. Zingatia kufanya kile ulichopanga kwenye orodha yako. 

Umuhimu wa kuwa kuwa na orodha ya vitu vya kufanya: 

1. Kutopoteza muda katika mambo yasiyo ya msingi. 
2. Kuwa na mwongozo unaokuongoza katika siku yako.
3. Kutumia muda wako katika vitu vyenye tija. 
4. Kuweka nguvu katika mambo machache yenye kuleta ufanisi. 
Wakati ndio huu kuweka orodha ya vitu vya kufanya ili siku yako iweze kuwa nzuri na yenye manufaa makubwa. 

Je, siku yako inaongozwa na nini? 

Bonga nasi hapa hapa 0767702659 

Lackius Robert 
#23mwangaza2023
 

Friday, February 17, 2023

Uchambuzi wa Kitabu Cha Where There is a Problem There is Money...

Katika kuendelea kuikuza Shauku. Nilipata nafasi ya kusoma, Kitabu cha  "Where There is a Problem There is Money" kilichoandikwa na Dkt. Sunday Adelaja mnaigeria mwenye mafanikio makubwa katika uandishi na uchungaji. Akifanyia utume wake mjini Kiev Ukraini. Katika kusoma kitabu hicho ndipo nilipokutana na neno "Air Ambulance Service au Flying Doctors Health Care" nikata kupata uelewa kwa ndani. 

Mwandishi Dkt. Sunday katika kitabu chake  anaelezea namna shauku ilivyo na nguvu kubwa kubadilisha maisha ya watu.  Anamwelezea Dkt. Ola Orekunrin mnaigeria aliyezaliwa mjini London Uingereza akiwa na shauku ya kuwa dakatari.  Kwa jitihada zake zote na kuufanikisha na akapata udaktari akiwa na umri mdogo. Mwandishi anasema alifanikiwa kuwa daktari akiwa na miaka 21. na kupata ufadhiri kusoma Japani na aadaye kurudi Uingereza kuendelea kazi. 

Dkt. Ola akiwa anaendelea na kazi zake za udaktari alipata taarifa kuhusu hali ya dada yake. Kuwa anaumwa ugonjwa wa "Sickle Cell Anemia" hali inayofanya kuishiwa damu muda mwingi. Hali hiyo ilimuumiza kichwa sana Dkt. Ola akaona ni bora afanye mpango wa kumsafirisha dada yake kwenda kupata matibabu katika nchi zilizo karibu. 

Usafiri uliokuwa unahitajika ulikuwa ni wa Air Ambulance yaani unasafri angani huku ukiwa unaendelea kupata matibabu. Maana yake ni kwamba wakati unapelekwa hospitali matibabu kwako yanaendelea bila shida. Na aina hizi za huduma wanapea watu waliozidiwa na ugonjwa. 

Kutumia usafiri wa ndege kutoka nchi moja kwenda nyingine kidogo inachukua muda mrefu kama hakuna matibabu ndani ya ndege inaweza kupelekea mgonjwa kuaga dunia. Kwa hiyo Dkt. Ola akafaya utafiti kwa nchi za Ghana, Sierra Leone, Cameroon na nchi zingine za Afrika Magharibi kuona kama itapatikana ndege hiyo au taasisi inayotoa huduma hiyo ili amsafirishe dada yake kutoka Nigeria kwenda katika nchi hizo lakini haiweza kupatikana. 

Katika utafiti akagundua ipo moja katika nchi ya Afrika ya kusini haraka haraka taratibu za kumsafirisha zikafanyika. Yakiwa yamebaki masaa matano taratbu zote kukamilika kwa baati mbaya dada yake akaaga dunia. Moja kati ya kitu kilichomuumiza sana Dkt. Ola 

Aliumia sio kwa sababu pesa haikuwepo bali kukosekana kwa huduma ya Air Ambulance ambay ni salama na haraka. Ni huduma inayokuwa na jopo la madaktari wenye vifaa mbalimbali kwa ajili ya kumtibu mgonjwa akiwa angani. Yaani kabla hujafika hospitalini tayari huduma za kimatibabu zinakuwa zinaenelea. Na hiyo huduma inaunguza saa vifo kwa sababu wagonjwa wengi wanakufa wakiwa safarini hasa katika maeneo ya vijijini na nchi zenye vita. 

Baada ya kifo cha dada yake Dkt. Ola alifanya maamuzi ya kucha kazi yake ya uuguzi katika nchi ya Uingereza na kuamua kwenda kwao nchini Nigeria kuona kama lipo jambo anaweza kulifanya kuzuia vifo vingi visitokee. Anasea kigfo cha dada yangu kimetokana na kukosekana wa huduma abayo tunaweza kuianzisha na kuwaponya wengi zaidi. 

Hapo ndipo  wazo la Air Ambulance Service au Flying Doctors Health Care likaanza kufanyiwa kazi. Aliamini likifanikiwa litawasaidia wengi sio tu katika nchi ya Nigeria bali Afrika Magharibi na Afria kwa ujumla. Kupitia wazo hilo aliona ili lifanikiwe ipo elimu za ziaa inahitajika kwake. Hivyo aliamua kusomea masuala ya huduma za angani yaani Air Ambulance Service na baadaye apata mafunzo ya urubani upande wa helikopita. 

Shauku yake kuu ilikuwa ni kuwasaidia wagonjwa wanaopata shida za kifaya katia nchi ya Nigeria na Afrika Magharibi kupata huduma haraka. Hakuendelea kuweka nguvu kwa dada yake bali aliona kuna haja ya kuwaponya wengi zaidi na hapo ndipo msemo wa usipoziba ufa utajenga ukuta unapofanya kazi. Aliona ni bora kuzuia vifo vingine kuendelea kutokea. 

Flying Doctors Nigeria Limited chini ya Dkt. Ola ndiyo taasisi ya kwanza kutoa huduma za haraka kwa watu wanaopata majeruhi na wenye uhitaji wa matibabu ya haraka Afrika Magharibi. Norman Vincent aliwahi kusema , “kila tatizo lina mbegu na suluhu yake. Kama huna tatizo hutakuwa na mbegu” na hiki ndicho tulichoona kwa Dkt. Ola. 

Dkt. Ola alinukuliwa akisema, chini nyingi za kiafrika zna changamoto ya magari ya ambulasi na hayo machache unakuta kuna changamoto ya barabara kuwa mbovu hali inayopelekea baadhi ya wagonjwa kuaga dunia wakiwa wanapelekwa kupata matibabu. Anasema, sikuja Afrika kuonyesha kwamba mimi nina utaalamu sana. Bali nilitaka kuja na suluhu inayoweza kuokoa maisha mengi ya watu. Sikuona haja ya kulalamika kwamba serikali haikuwa imewea mkazo au kulalamikia barabara zetu. Niliona nifanye kile kinachowezekana kufanyika kuwaokoa wenzetu. Changamoto zilikuwa nyingi, makosa na vizuizi vigi lakini tulifanikiwa. 

Dkt. Ola amepewa tuzo mbalimbali, ameajiri wafanyakazi zaidi ya 30 na kwa na ndege zaidi ya 20 zinazotoa huduma ndani na nje yaNigeria. Amekuwa mhamasishaji bora na mjasiriamali mkubwa kwa sasa lakini yote hiyo imetokana na shauku aliyokuwa nayo kuwa daktari na kuwaponya wengi zaidi. 

Maana ya flying doctor hawa ni madaktari wanatoa huduma za kiafya huku mgojwa akiwa kweye ndege au katika maeneo yaliyo mbali na huduma au yaliyotengwa. Mfano wakati wa vita kunakuwa hakuna  huduma boraza kiafya hivyo wanachukulia madaktri kwenda katika maeneo hayo kutoa huduma. Wanakuwa na vifaa vya kutosha kuwapatia tiba wagonjwa katika maeneo yao. 

Ndugu yangu mpendwa unautumiaje muda wako? Je, unatafuta sababu za kujificha kwenye makosa? Sikia hii; kama wewe sio sehemu ya suluhu bali ni sehemu ya tatizo. Wakati ni sasa ni malengo mengi umepanga usiendelee kuwa mtu wa kulaumu serikali ndugu jamaa na marafiki. 

Hayo ni machache katika kitabu hicho tuwasiliane upate uchambuzi kamili. 

Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659
#22mwangaza2023

Thursday, February 16, 2023

Unajua nini kuhusu?....

Kama upo kwenye biashara au unatoa huduma yoyote kwa maana unapokea malipo au unafanya mauzo. Basi ipo njia sahihi ninayotaka kukushauri leo. 

Ukweli ni kuwa, tumekuwa tukiingia kwenye malumbano na wateja wetu mara kwa mara. Moja kati ya sababu inayopelekea sisi kuingia kwenye malumbano hayo ni pale tunapobishana na mteja. 

Kitu kimoja usichokijua ni kuwa pale mteja anapokuja kwako kwa ajili ya huduma au biashara. Kuna eneo analokuwa amejiwekea ukomo. Hii haijalishi anaijua bidhaa au biashara yako.

Inapotokea wewe ukaenda nje ya ukomo huo lazima akatae. Sio tu kukataa lazima akupinge. Wakati mwingine anatafuta sababu nyingi ili aondoke bila kuchukua bidhaa. Usipokuwa makini utajikuta unalumbana na kila mteja.  Na yeye anaamini yupo sahihi hata kama sio. 

Hivi, unakumbuka siku alipokuja mteja anahitaji huduma yako. Ulivyoanza kumuelezea akaanza kukubishia? Imagine wewe ndiye mwenye biashara au unayotoa huduma halafu anakubishia. 

Ulipomwambia inafanya vizuri sana. Akakwambia, tena hii bidhaa au huduma niliwahi kuitumia ni mbovu. Au nimeambiwa haidumu kwa muda mrefu. 

Hope, unakumbuka ulimbishia sana. Hali iliyopelekea sintofahamu. Ulipotoka pale ukasema yaani huyu bwana! kaniharibia siku. Ukatamani kufunga duka au kusitisha huduma.

Ipo namna nzuri kutumia. Pale anaposema huduma mbaya. Bidhaa aifanyi kazi muulize hivi, unajua nini kuhusu? ...mfano unauza vifaa vya spear. Mteja anasema vifaa vyako vibovu. Unamuuliza hivi; je, unajua nini kuhusu spear za JK? Au unajua nini kuhusu huduma ya delivery? Hapo atatoa maelezo mengi. Akiwa anaamini ni mshindi. 

Akiwa anaelezea, msikilize kwa makini. Usimkosoe au kumwambia umevurunda. Wewe msikilize kisha msahihishe eneo analokosea. Kiupole sana. Mwambie, sasa hivi tunatoa huduma ya delivery au spear za JK zinafanya hivi na vile. Kumuuliza aseme mwenyewe kuna vitu atagundua anavikosea na kuwa tayari kukusikia. 

Ukielezea vizuri utaona anaanza kuzunguka oh! Unajua hivi ama vile. Basi nitakuwa nadanganywa au basi nipe nijaribu nione na vitu kama hivyo. 

Itumie hiyo kila unapokutana na mteja anayelalamikia huduma yako. Muulize kwa upole kabisa. Je, unajua nini kuhusu?......kaa kimya msikilize. Hii njia inaondoa malumbano kwa kila aina. 

Unajua nini kuhusu branding? 
Unajua nini kuhusu tlanslation, Ndoto yako, Maendeleo binafsi, ustawi wa biashara, uaandaji wa proposal, project, ubunifu, mauzo na mengine mengi kutokana na huduma unayotoa. 

Na mimi nikuulize je, unajua nini kuhusu mauzo, kusudi au ndoto Ya Maisha Yako? 

Ni kipi kingine ungependa tuzungumzie?

Bonga nasi hapa hapa 

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#21mwangaza2023. 

Wednesday, February 15, 2023

Usifuate mkumbo..

Hakuna maisha yanayotesa watu kama ya mkumbo. Haya ni maisha unayopaswa kuyakataa. Ni maisha yaliyowapoteza wengi. Wapo walioona marafiki zao wanamiliki magari, wakaamua kukopa pesa na kwenda kununua magari. Baada ya muda mfupi, magari yakaharibika na wakajikuta wanaishi kwa shida kujificha huku wakiwa na madeni makubwa.

Unapaswa kujua kuwa, kila mmoja anayo riziki yake. Inapokuja hakuna anayeiondoa au kuirudisha nyuma. Kila mmoja namna anavyoishi anajua mwenyewe. Kupata kwake, kukosa kwake, anajua mwenyewe. Kitu kisichoonekana usoni mwetu ni matatizo, madeni, machungu na maumivu tuliyonayo. Siri ya moyo yetu aijuaye ni kifua. Mtu asipokwambia anayopitia, huwezi kujua.

Kuna wakati najiuliza kama ingetokea matatizo au nyakati ngumu tunazopitia au matendo tunayofanya yangejionyesha
usoni. Yaani unaona usoni mwa fulani mwizi, kahaba, mchezaji, msanii, tajiri, maskini, mchawi au mfukoni hana hata kumi. Hii ingekwa changamoto kubwa. Huenda tungeishi maisha yetu halisi kwa sababu hakuna anayeweza kufuata matendo mabaya yanayofanywa na mwenzake.  Inapotokea tumekosa, tusingeweza kuwatembelea ndugu au watu wa karibu maana wangejua kile tulichofanya.

Umemuibia mtu usiku akikutana na wewe mchana usoni mwako kunaonyesha kile ulichofanya. Anakukamata na kukuchukulia hatua. Lakini yote hayo hayajawa hivyo. Kila mmoja anajua namna anavyopata mahitaji yake.

Unachotakiwa ni kuishi maisha yako mwenyewe. Kama hujui mtu amepataje kitu, usilazimishe kuwa kama yeye. Huachi alama kwa kuishi kama fulani bali unaacha alama kuishi kama wewe. Fanya kile unachoona ni sahihi kwa ajili yako na jamii yako. Usifanye kwa ajili ya fulani. Hutoweza kupata furaha wala kutimiza lengo uliloweka kwa sababu hamasa
kiutendaji itakuwa ni ndogo. 

Wakati ndio huu kuweka mikakati mzuri juu ya kitu unachofanya ili baadaye uwe yule unayemtaka. 

Inawezekana sasa.

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#20mwangaza2023

Tuesday, February 14, 2023

Jinsi kitabu cha Think and Grow Rich kilivyokuza shauku yangu

Mwaka 2019, wakati nafanya uchambuzi wa kitabu cha Think and Grow Rich chake Napoleon Hill nilipata mshangao mkubwa. Moja kati ya vitu alivyoandika ni shauku aliyokuwa nayo bwana mmoja Edwin C. Barnes. Bwana huyu alikuwa na shauku kubwa ya kuonana na kufanya biashara na  mgunduzi wa bulb za umeme Thomas Edison. Katika kitabu hicho mwandishi alijarbu kuonyesha namna gani mtu anavyokuwa na shauku na inavyomsaidia kufanikisha malengo na mipango yake. 

Anasema, akiwa anaelekea ofisini kwa Thomas Edison akili yake ilikuwa kazini. Alijihisi mwenyewe kama vile tayari alikuwa mbele ya Edison. Alisikia sauti ndani mwake ikimuomba Bwana Edison fursa ya kutekeleza jukumu zito katika maisha yake. Shauku yake ni kuwa mbia kibiashara na mgunduzi  huyu mkubwa. Alipofika mbele yake alikuwa na furaha kubwa na hapo aliona shauku yake imekuwa kweli. 

Miaka michache baadae alikuwa katika biashara na Edison. Shauku iliyokuwa imetawala katika maisha yake ilikuwa imegeuka kuwa kitu halisi.
Waliokuwa  wanamfahamu Barnes walianza kumuonea wivu kutokana na mafanikio aliyojaliwa maishani. Waliona katika siku zake za furaha, bila ya hata kujisumbua kuchunguza sababu za mafanikio yake.

Barnes alifanikiwa kwasababu alichagua lengo dhahiri, na akaelekezea kwalo nguvu zake zote. Matumaini yake yote pamoja na jitihada zake zote katika kulitimiza lengo hilo. Alikuwa yuko radhi kuanza na kazi ya chini kabisa, ilimradi tu kazi hiyo ingempatia japo fursa ya kupiga hatua moja kuelekea lengo alilokuwa amelipanga.

Ilikuchukua zaidi ya miaka mitano kabla hajafanikiwa kuipata nafasi aliyokuwa akiitafuta. Kwa kipindi chote hicho hakuwa na mwanga wowote wa matumaini, wala ahadi moja ya kufikiwa kwa shauku yake. Kwakuwa ni kitu kilichokuwa ndani ya moyo wake aliamua kujipa motisha mwenyewe. Katika akili yake alikuwa anajiona yupo mbele ya Edison kwa kila sekunde iliyokuwa ikipita. 

Kufanikisha lengo lake alitumia kauli isemayo “nitayaunguza madaraja yote nyuma yangu na kuweka rehani mustakabadhi wa maisha yangu na kupata ninachokitaka”  Alichokuwa anataka ni kuonana na kuingia ubia na Thomas na hilo ndilo wazo kuu alilokuwa awaza muda kwa mrefu.

Alipokuwa akienda kuonana naye hakusema, “nitajaribu kumshawishi Edison anipe kazi ya aina fulani”. Ila  “nikimuona nitampa ujumbe kuwa, nimekuja kuingia naye ubia wa biashara” hapa tayari alikuwa na mpango ulio tayari ni kitendo tu cha Thomas kuupitiana kufanya maamuzi. 

Hakusema, nitafanya kazi pale kwa miezi kadhaa ikiwa kama sitapata motisha, nitaacha na kutafuta kazi mahali pengine. Bali nitaanza popote, nitafanya chochote atakachoniambia nifanye. Ila ninachotaka ni kuwa mbia naye kibiashara na sio jambo lingine. 

Unaweza kuona namna gani ndugu yetu Barnes alivyokuwa amejipanga. Aliweka mipango sawa hakusubiri kufika kwa Thomas na kutafuta fursa. Bali alienda nayo kazi ibaki kwa Thomas kufanya maauzi. Alienda amedhamiria kufanya kila kitakachoweza kumkutanisha na Thomas ili mradi apate nafasi ya kuonana naye. Na hatimaye, alifanikiwa kupata kile alichokihitaji na kufanya kazi pamoja na Thomas. 

Barnes, hakuruhusu hali ya kutowezekana au hofu ndani yake. Unaweza kuona muda aliochukua hadi kufika mbele yake zaidi ya miaka mitano. Na hapo hakupewa hamasa wala neno la faraja kutoka kwa watu wengine. Badala yake walimuona kama mcheza sinema. Ila yeye pekee ndani yake ndiye aliyekuwa anajua ni nini anahitaji. 

Hapo ndipo tunaposema una machaguo mawili aidha ushinde au ufe. Kama vitani vile, ukiwa vitani hakuna kurudi nyuma. Huna cha barabara mbovu, maji mengi chakula hakuna au huoni mbele kazi ni moja tu upige au upigwe. Yote hiyo itategemea namna ulivyojipanga pamoja na shauku iliyo ndani yako. 

Shauku ni dira yako. Inatoka ndani yako kadiri unavyokuwa na shauku kubwa ndivyo unavyoyaandaa mafanikio makubwa ndani yako. 

Huwezi kuwa Barnes ila yapo masuala utajifunza na kuyafanyia kazi katika mambo yako ya kila siku. 

Kwa maelezo zaidi pitia uchambuzi wa kitabu hiki kwa kubonyeza hapa chini 


Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659 
#19mwangaza2023

Monday, February 13, 2023

Njaa waliyonayo wengi wetu...

Dunia tuliyomo inayo mambo mengi. Kadri siku zinavyozidi kusogea ndivyo mambo yanavyozidi kuwa makubwa. 

Na ndani yake kuna matukio yanayojitokeza kila siku. Kutokana na uwepo wa matukio hayo yanayokuja na matokeo tofauti. Wengi wetu tumejikuta tunaweka nguvu kwenye vitu vyetu. 

Ukitaka kujua hili, nenda na mwenzako mahali. Piga picha naye alafu mtumie picha ambayo hayupo. Kisha mwambie umependeza akusaidie kuipost hapo Mtagombana. Umimi umeanza kushika hatamu. Hadi imefikia point msaada pakee unaoweza kuupata ni "pole sana".  Hope unanielewa na wewe ni shaidi

Hii hali imepelekea hata watu kushindwa kuwasifia hata baada ya kufanya kitu kizuri. Lakini moja ya siri kubwa ninayokupa leo ni hii. Kumsifia mtu baada ya kufanya kitu kizuri au maamuzi sahihi. Ni eneo linalomfanya mtu afurahie zaidi. 

Hii inamfanya aweke umakini kwako. Pata picha umeenda dukani kununua vitu vyenye thamani ya elfu hamsini. Muuzaji akakwambia hongera sana kuchukua vitu vyenye thamani ya pesa nyingi sio wengi wanamudu. Au hongera kuchukua hatua kununua simu nzuri, gari, pikipiki, nguo au kiatu. Unasikia furaha isiyo na kifani. Hadi unatamani kumpa buku la ziada..

Kwa taarifa yako. Hii ndio njaa waliyonayo wengi wetu. Unaenda kukutana na Bosi, mme/mke, Boy/girl friend wako. Ile unafika mbele yake. Unamwambia aise! Hongera sana  Robert/Glory, umependeza sana hicho kiatu au shati limebamba, mmmh! hizo nywele zako hatari sana. Utaona anatabasamu. 

Hivi unafikiri hakuna anayetaka kufisiwa? Hayupo kila mmoja anapenda. Na hii ndio njaa waliyonayo  wengi wetu.
Wakati ni sasa. Mwambie hongera kwa maamuzi mazuri uliyofanya. Mme/mke wako mzuri sana. Nyumba yako, gari yako, tisheti yako nzuri sana. Hongera sana

Mtu anaposifiwa hata kama sifa ni ndogo inamfanya mtu anajisikia vizuri. Sasa ni nini unaenda kumsifia? Hapa unaangalia namna alivyo mfano nguo. Amevaa jezi ya Mnyama au mwananchi. Unaanzia hapo, ikiwa ananunua kitu msifie mwambie hongera sana kwa kuchukua hatua. Kununua vifaa hivi, sio wote wanaweza kumudu gharama. 
Unapofanya hivyo na yeye kichwa chake kinavimba na anaanza kukusikia. Uzuri kwenye kusifia huwezi kukosea. Wewe unaongea na mtu unayemtazama.

Lengo kuu ni kutaka kuongeza umakini na usikuvu mkubwa kwenye kile mnachoenda kuzungumzia. Kumsifia mtu kunakusaidia kuwa na pa kuanzia. Maana unapomsifia lazima ataongea. 
Nikuulize je, hutaki kusifiwa? Bonga nasi hapa hapa.....

Imeandaliwa na Lackius Robert 
#18mwangaza2023.

Sunday, February 12, 2023

Huwezi kukwepa ujasiri

Tunaposema ujasiri maana yake ni hali ya kutenda jambo bila kuogopa. Kwa lugha rahisi bila kuwa na wasiwasi wowote.

Kwa bahati mbaya ujasiri sio jambo la kurithi kama tulivyozoea katika baadhi ya vitu. Ni zao unalolizalisha mwenyewe kutokana na jambo unalofanya. Ikilinganishwa na matokeo unayohitaji kuyapata. 

Ikiwa hutakuwa na ujasiri katika utendaji wako basi ujue hata kufanikiwa itakuwa ngumu. Maana mafanikio yenyewe ni ujasiri tosha.

Kuna wakati utasimama uso kwa uso na mlima mrefu unaohitaji ujasiri kufanya maamuzi. Juu ya gharama kiasi gani inahitajika kuupanda. 

Una biashara, kila mmoja atakuja na maoni yake. Kwanini usiongeze hiki. Mwingine kwanini usipunguze hiki. Kwa nini usikope kiasi fulani benk uongeze hiki au kitu kingine. Bila kuwa na ujasiri hutaweza kukwepa hali hiyo. 

Unahitaji kumpata mwenza wako. Lazima uwe na ujasiri wa kuyakwepa mapingamizi ya watu wako wa karibu. Maana kila mmoja atakuwa na ushauri juu ya mtu huyo. Kuna watakaosema, tafuta mwenye level fulani ya elimu. Mwenye kazi, biashara au kutoka katika kabila fulani. Yote hayo bila kuwa na ujasiri utapata shida katika maamuzi. 

Hivyo basi, ujasiri ni hitaji muhimu kwa mwanamafanikio yeyote. 
Kuongozi lazima uwe jasiri kuwaongoza wafuasi wako. 
Mchungaji lazima uwe jasiri kuwachunga kondoo wako. 
Msanii lazima uwe jasiri kuwaburudisha wafuasi wako. 
Mwalimu lazima uwe jasiri kuwafundisha wanafunzi wako. 

Bila kuwa jasiri utabaki njia kuu. Woga, hofu na lawama vitakujaa. 
Wakati ndio huu. Kama sio sasa ni sasa. 

Je, wewe ni jasiri katika kazi yako? 
Bonga nasi hapa hapa.

Imendaliwa na Lackius Robert 0767702659 
#17mwangaza 2023

Saturday, February 11, 2023

Moja inakutosha?

 Ni swali ambalo nilimuuliza, mmoja wa watu naowafanyia training kwenye program zangu. Yeye yupo kwenye mauzo kwa maana ya biashara. Nilihitaji apate pia, huduma nyingine kati ya ninazotoa. 

Kabla hajaanza program aliniambia, ndoto yake kuu ni kuwa muuzaji bora. Kuongeza ushawishi mkubwa katika biashara yake. Kuna vitu vingi alinielezea vinampa shida. Nikamwambia "mauzo sio kitu cha siku moja bali ni kitu chenye mkusanyiko wa vitu vingi ikiwemo kujifunza kila siku".

Ni mengi tuliongea lakini, moja ninalotaka kukushirikisha leo ni hili. Limekaa kama swali lakini lina nguvu kubwa unapomwambia mteja. 

Ni kweli program aliyokuwa anataka nilimpatia. Lakini kwa kuwa zipo nyingine, sikusubiri aulize baada ya kukubali ya kwanza. Nilimuuliza hilo swali. Akashaangaa kidogo, baadaye akasema kama ipo nyingine inayoendana na hii nipe Kaka. 

Mpaka sasa amekuwa akilitumia mara nyingi zaidi katika hudhma zake. 

Sasa wauzaji wengi wamekuwa hawalitumii mara baada ya kumuuzia mteja. Tafiti zinaonyesha ukilifanyia kazi kwa wateja wengi wapo wachache utawafanikisha. 

Ipo hivi pale unapokuwa umemuuzia mteja kitu. Au unazo huduma labda za mafunzo unazitoa. Mteja akaja na kuhitaji bidhaa moja. Usisubiri hadi akwambie nataka kitu kingine. Wewe muulize je, moja inakutosha? 

Unapokuwa umemuuliza hili maana yake yeye atakwambia ikiwa anahitaji au la. Epuka kujipa majibu. Wewe kazi yako ni moja. Na swali hilo ni je, moja inakutosha. Wewe mwambie kila anayekuja kupata huduma kwako. 

Mfano unafanya uandishi, tafsiri na printing. Mteja akihitaji huduma ya kuandikiwa mwambie moja inakutosha. Ikiwa na maana mpatie huduma nyingine. 

Point yangu ni kwamba, wewe timiza wajibu kumuuliza hilo swali. Kila mteja unayekutana naye katika huduma yako. Usiache akachukua huduma yako bila kumuuliza. 

Tahadhari: Usimuulize kabla hajafanya mauzo. Subiri akamilishe mauzo ndipo umuulize. Ili umhudumie zaidi. 

Na mimi nakuuliza ndugu yangu mpendwa. Makala hii inakutosha? 

Bonga nasi hapa hapa 

Imeandaliwa na Lackius Robert  0767702659

#16mwangaza2023. 


Friday, February 10, 2023

Ungepita njia hii?

Ilikuwa majira ya asubuhi, Rama akiwa anaendesha gari kuelekea kazini. Ni muda ambo alikuwa anawahi kazini kwenye kikao na wakurugenzi. Rama alikuwa anaendesha gari alilopewa na ofisi ili kuongeza ufanisi kwake ikiwemo kuwahi kazini. 

Siku hii kulinyesha mvua kiasi. Baadhi ha njia zikawa na foleni. Sasa wakati Rama aneendesha alifika sehemu iliyomshangaza kidogo....

Ukiachana na Main Road kulikuwa na njia ya chocho, ambayo magari mengi yalikuwa yanapita. Huku nyingine hakuna gari lolote lililokuwa linapita. Akajiuliza sababu na kuikosa. Na jana yake wakati anatoka kazini ndiko alikopitia. Rama akaanza kujiuliza juu ya nini afanye. Awafuate wengine au ajitose kwenye njia ya peke yake.  

Wakati anawaza zikaja gari nne nyuma yake na zote zikapita kwenye njia nyingine ya chocho. Kwa kuwa aliona magari yote yanapita katika njia hiyo. Bila kuuliza na yeye akaamua kuungana nao. Dakika chache baadaye simu ikaita bosi wake anauliza kama amefika. 

Rama: Helow! Boss!huki akiwa ameshika kichwa afanye nini, kule alikoingia gari nyingi hawezi kutoka tena. Njia ni ndogo. Kwa sababu kila mtu alikuwa anapita katika njia hiyo. 

Bosi: Uko wapi kijana wangu? 

Rama: Mhh! Yaani! Unajua Bobosii! Nipo hapa sio mbali na barabara kuu. Kuna chocho tumeingia kuna msongamano wa magari. 

Boai: Msongamano wa magari? Mhh mbona dakika chacha nimetoka huko hamna foleni. 

Rama:Sasa kilichotokea, nilifika kwenye kinjia pale kati nikaona watu wote wanapita nikaacha Main Road nikaunga. Japo niliwaza kitu kama hicho kukazania main road. Ila baadaye nikaona magari mengi yanapita njia hii nikaliunga. Kwa hiyo tunafanyaje bosi? Bosi: Nadhani huu mradi tushaukosa ila wewe ndio responsible. 

Ndio maana tulikupa gari ili uwahi. Ni nini umefanya? Muda wa kikao umefika. 

Rama: Mhhh hapana bosi..je, naweza kukuuliza? Boss ndio kijana wangu. 

Rama: Ingekuwa ni wewe, unaona watu wote wanapita njia ya chocho. Huku Main Road hakuna anayeendelea kwenda mbele ungepita njia hii? 

Bosi:Mhh ngoja kwanza nimeitwa ntakucheki baadaye. 

Rama: Helow Boss Helow boss. 

Sime imekatwa. Hakuweza kutoa jibu. 

Sasa kwako mpendwa msomaji. Ingekuwa ni wewe ungepita njia hii? 

Nini tunajifunza?

Kwanza hapo juu bosi alikata simu. Kwanini alikata simu? Swali aliloulizwa na Rama lilimpa utata sana. Aliona mazingira yalivyo. Ili kuyaepuka akakata simu. 

Ila Rama hakuuliza kujua kwa nini njia kuu haipitwi na hakuna kibao kinachoonyesha njia imezuiwa. Hivi ndivyo tunavyokutana na vishawishi maishani mwetu. 

Kumbe, kwenye maisha kila mtu anazo njia zake. Anayo safari yake. Anayo matarajio yake. Ikiwa huna yako, jua utaenda kukamilisha ya wengine. 

Chocho lako lipo katika kazi zako, familia yako, biashara yako. Lakini ili uyashinde yote haya. Baki njia kuu. Wengi wanapenda sana njia za mkato. Na unapofika kule kujitoa sio kazi ndogo. 

Wakati ndio huu kubaki katika njia kuu ambayo wengi wanaikataa. Ni njia iliyowazi kumfanye yeyote aliyejipanga kufikia hatma ya safari yake. Karibu tupite wote njia kuu. 

Mungu akubariki sana. Karibu tujifunze zaidi. 

Bonga nasi hapa hapa 

Imeandaliwa na Lackius Robert. 0767702659

Mwangaza2023

Thursday, February 09, 2023

Siku yako inalipa?

Kila siku huwa inanza tofauti. Fikra, hamasa au motisha ya jana huwezi kuifananisha na leo. Pata picha ni siku mpya imefika huku ukiwa huna mpango au ratiba yoyote. Ni nini kinakujia kwa haraka haraka akilini? Na unaionaje siku hiyo? Hakika jibu linachanganya sana. 

Kwa lugha nyepesi lolote litakalotokea kwako litakuwa kipaumbele. Na utaliona lina uzito. Kwa sababu hakuna mbadala wake.  Mwisho wa  siku utagundua siku yako  imekuwa ngumu, ndefu na imebana sana. 

Upande wa uzalishaji au matokeo utaona hayaridishi. Mengi yamefanyika, safari nyingi zimefanyika. Lakini tija ni kidogo. Kwa nini uligusa kila kilichokuja mbele yako. Kukianza litakuwa suala moja kukimaliza nalo pia litakuwa lingine. Na utaona ni sawa maana hamna mpangilio wowote unaokuongoza. Na itakuwa ni ngumu kufanya tathimini kwa kuwa huna mwongozo..

Hayo siyo maisha unayopaswa kuyaishi ndugu yangu mpendwa. Weka nguvu kubwa katika kuwa na mipango(to do list) kuendana na kile unachofanya. Kupitia mipango yako ndipo utaweka vipaumbele. Kwa maana ya kipi kianze na kipi kifuate. 

Natumaini umewahi kuisikia kanuni ya Pareto ya 80/20. Ikisema asilimia 80 ya matokeo unayopata yanatokana na asilimia 20 za juhudi zako. Hapo unaweza kuona, ukifanya vitu vichache vyenye tija vinaweza kukusaidia kupata matokeo makubwa. Kuliko kufanya vitu vingi visivyokuwa na tija. Swali la kujiuliza ni je, inalipa? Kile unachofanya kinachangia nini kufanikisha vipaombele vyako? Ikiwa ni hapana kiweke pembeni. Kama ni ndio hongera. Kifanyie kazi tena kwa upendo mkubwa. 

Hujachelewa, wakati ndio huu. Ipangilie vema siku yako, ili ikusaidie kufikia ndoto kubwa za maisha yako. "Ikiwa huna kitu, usiogope kwa unachokipoteza". 

Je, ni nini ungependa tukusaidie katika kuweka mipango au vipaombele?

Bonga nasi hapa hapa

Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659


#1mwangaza2023

Wednesday, February 08, 2023

Unavyoitafsiri dunia sivyo..

 Unavyoitafsiri dunia sivyo...

Mafanikio yako yapo katika kile kitu unachotaka kuwa au kufanya. Na sio anachofanya mtu mwingine. Kama unataka kuwa mtu wakuandika unapaswa kuyaishi maisha hayo. Kama wewe ni mfanya biashara na ndiyo maisha unayoyataka, basi unapaswa kuishi katika hali hiyo. Na sio  kwamba waimbaji, wachezaji au walimu ndio hufanikiwa. 

Maana kitu unachokiwekea nguvu na kukifanya kila siku ndicho kinachokufanya uwe na amani na furaha.

Kama wewe ni mtu wa kuimba ukiishi mziki na ukaishi maisha ya uchezaji mpira kuna kitu kwenye maisha yako hakitaenda sawa. Yaani hutopata matokeo mazuri. Kuna kimoja kitakuwa na matokeo mazuri kuliko kingine. 

Ili uweze kuwa mtu wa mafanikio unapaswa kuyaishi maisha ya kitu unachotaka au unachofanya. Ikiwa umeona kinaweza kukuvusha. Weka nguvu katika kitu hicho. Fanya kinachowezekana kukifanikisha. Jifunze na kuwapenda watu waliofanikiwa na kitu hicho. Tofauti na hapo hutofanikiwa.Usiache pia, maeneo mengine  kufuatilia na kujifunza zaidi.

Katika maisha yangu nimejifunza kuwa; ili uweze kufanikiwa unahitaji kitu kimoja kwanza. Ambacho kitakuvusha kutoka sehemu moja hadi nyingine. Yaani iwe mchana au usiku. Wakati na masika wakati wa kiangazi. Unakifanya kweli kweli. Kila unapoamka asubuhi fanya kile kitu ulichochagua. Mfano angalia "Google" inahusu "search" kwa maana ya kutafuta. Wao waliwekeza hapo. Na ndiyo kilichowavusha waanzilishi. Angalia Apple, Amazon na zingine. 

Kwani ukiamka asubuhi mipango yako inahusu kitu ulichochagua? Na vipi kuhusu ratiba zako? Mizunguko yako na watu wako wa karibu?

Kama huwezi kufanyia kazi kitu unachokitaka kwa kujituma mafanikio utayasikia kwa watu. Na hapo utabakia na tafsiri yako kwamba; dunia ni ngumu au maisha ni magumu. Kumbe ugumu unauweka wewe. Kwa lugha nyingine wewe mwenyewe ndiye unayejizuia. Ukifanya kazi zako kwa bidii kila siku na ukatumia muda wako vizuri maisha yako yatabadilika na kuwa mazuri. 

Swali: Kitu kipi kimoja unakifanya bora kuliko kingine? 

Bonga nasi hapa hapa

Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659

#13mwangaza2023.

Tuesday, February 07, 2023

Ni siku nzuri au mbaya kwako?

 Ni swali unalopaswa kujiuliza kila mara uamkapo asubuhi. Maana namna unavyoanza siku yako ni kiashiria tosha kuwa itakuwa nzuri au mbaya. Unaweza kuanza na maombi, tahajudi au mazoezi, kusoma kitabu au kusikiliza redio au mafundisho mazuri yenye hamasa chanya. Kutenga muda asubuhi kujifunza kitu ni muhimu sana, maana itakupa nguvu na kuiangaza siku yako. Japo baadhi yetu hatufanyi hivyo. 

Mwingine ukimwambia kuhusu maombi ya asubuhi, kumshukuru Mungu kwa kumpa nafasi kuona siku nyingine, anaona kama unampotezea muda. Lakini ni muhimu sana kwa mtu mwenye maono makubwa. Muda wa asubuhi ni mzuri sana kupangilia ratiba zako. Hasa hasa baada ya kuwa umepata hamasa kupitia vitu mbalimbali. Binafsi mawazo mengi mazuri huwa ninayapata asubuhi. Hii ni kwa sababu akili yako inakuwa mpya ina nguvu haijavurugwa na kitu chochote, ukiachana na ndoto za usiku. 

Najua umewahi kusikia msemo huu; “umenikuta na akili zangu za asubuhi”. Maana yake umenikuta nipo timamu, sijapigwa na jua, kuvurugwa na usafiri, baba mwenye nyumba au bosi wangu kazini. Akili inakuwa na uwezo mkubwa wa kufikiria. 

Watu wengi waliofanikiwa huwa wanatumia sana muda wao wa asubuhi kupangilia ratiba za siku zao. Katika hili sio lazima utumie muda mwingi sana. Oh! Et masaa manne au matatu. Unaweza kutenga hata dakika 30 au zaidi pengine saa moja kulingana na unavyotaka wewe. Labda kuanzia saa kumi hadi saa kumi na moja asubuhi, au saa kumi na moja asubuhi hadi saa kumi na mbili asubuhi. Wewe tu kulingana na uchaguzi wako. 

Safari ya maili elfu moja huwa inaanza hatua moja. Mafanikio ya wiki, mwezi au mwaka, vyote hujengwa kuanzia siku moja. Ambayo ndio kama hii uliyoamka asubuhi ya leo. 

Yule unayemuona amefikisha miaka mia moja alianza na siku moja. Aliye juu ya mlima hajaibuka tu kupanda mlima, bali alijipanga na kufanya mazoezi aliyokuwa anafanya kwa siku moja. Mchezaji maarufu alianza na mazoezi ya siku moja. Mwandishi maarufu kadharika na wengine. 

Leo ni leo amua ufanye kitu. Hakika lilo jambo utalibadili. Ikiwa kuna changamoto tuwasiliane 0767702659. 

Mimi nimeanza na hii ☝️ wewe je? 

Bonga nasi hapa hapa...

Imeandaliwa na Lackius Robert 

#12mwangaza2023.

Monday, February 06, 2023

Hivi sivyo hukutoa kwenye dira?

 Hivi sivyo hukutoa kwenye  dira?

Ebu chukulia mfano kwenye hosptali Daktari amshafishe  mgonjwa, amsikilize, apige simu na  wakati huo amhudumie  mtu mwingine kwa kumpatia madawa. Baada ya hapo afanye ukaguzi wa list ya malipo yanayopaswa kufanyika. Daktari huyo huyo awafuatilie wagonjwa wengine wanaosubiri huduma. Kwa hali yoyote lazima atafanya makosa kwa mmoja au kukosea kwa wote, either katika kutoa dawa zisizo sahihi au kushindwa kumuosha vizuri mgonjwa mwingine. 

Halikadharika sisi, Kila wakati tunapokuwa tunafanya kitu zaidi ya kimoja tunakuwa tunagawanya mazingatio yetu au nguvu zetu. Katika sehemu nyingi. Hali inayotupeleka nje ya dira yetu. Ni sawa na ule msemo wa “huwezi kuwatumikia mabwana wawili kwa wakati mmoja”. Ikiwa hutawakosa wote bali utamkosea mmoja na kumfanyia usahihi mwingine. 

Utafiti uliowahi kufanywa na taasisi moja  ulionesha matokeo ambayo mtu anayefanya kazi nyingi kwa wakati mmoja anaweza kuyapata;

i. Kupoteza ufanisi. Yaani hapa kazi yako inakuwa haina ubora ule unaotakiwa. Maana nguvu zinaenda katika vitu vingi ndani ya muda mmoja.

ii.Kadri unavyotumia muda mwingi kufanya zaidi ya kitu kimoja ndivyo unavyopata matokeo kidogo maana hujaweka nguvu kwenye kitu kimoja.

iii. Unapoteza zaidi ya asimilia 28% kufanya vitu ambavyo vinapunguza ubora na ufanisi wetu. Pale ambapo unakuwa unafanya vitu vingi kwa wakati mmoja.

iv. Muda unaoutumia ni mwingi kulingana na kitu husika. Badala ya kufanya kitu kimoja kwa wakati ukakimaliza unaenda kufanya kitu kingine. Wewe unafanya vyote kwa pamoja kitu kinachopelekea kuchelewa kumaliza kwa wakati.

v. Makosa. Watu wanaofanya kazi nyingi kwa wakati mmoja ni rahisi kukosea au kufanya makosa mengi 

kuliko wale wanaofanya vitu vichache vya msingi.

vi. Msongo wa mawazo (stress) watu wanaofanya kazi nyingi kwa wakati mmoja wanasumbuliwa sana 

na msongo wa mawazo maana vitu vingi wanakuwa hawajavimaliza kwa wakati. Anawaza hiki mara kingine kinamjia. Yote hayo yakiungana yanatengeneza kitu kinachoitwa stress ambayo hupoteza furaha ya mhusika.

Zingatia hizi big idea;

1.Usijisikie vibaya ukutanapo na miingiliano yaani distraction maana kila mtu anakutana navyo. Wewe weka nguvu katika vitu vichache vya muhimu kuzingatia dira yako.

2.Usiruhusu miingiliano itawale kazi zako maana inapoteza concentration, furaha na vitu vinginevyo.

Kufanya vitu vingi inawezekana lakini haviwezi kuwa na ufanisi mzuri chagua kitu kimoja kifanye vizuri. Kisha fanya kingine au tenga muda. Vipe nafasi kulingana na uharaka lakini sio kwa wakati mmoja ili usitoke nje ya dira yako. Lengo kuu ni kutotoka nje ya dira yako na kuwa na ufanisi mkubwa.

Ikumbuke kanuni ya Pareto ya 80/20. Asilimia 80% ya matokeo inatokana na asilimia 20 ya juhudi. Ikiwa na maana vitu vichache vyenye tija hukupatia matokeo makubwa. 

Je, wewe upo kwenye dira yako? 

Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659

#11mwangaza2023.

Sunday, February 05, 2023

Fanya kwa moyo wako wote

Fanya kwa moyo wako wote..

Ili uwe na mafanikio kikazi au hata masuala mengine huhitaji miujuza, maombi au mfungo. Kwamba mpaka ukoo ufunge maombi ya siku 7 au zaidi ili kazi au mambo yako yafanikiwe. Huku wewe ukiwa mahali umetulia, unasubiri fulani aamue au kufikiria kwa niaba yako.

Bali unahitaji kufanya kazi yako au mambo yako kwa moyo wako wote. Kwa uwezo wako wote na kwa namna unavyoona inafaa. Sasa changamoto ambayo imekuwa inatukumba walio wetu ni ile hali ya kufanya kazi au kitu pale tunapojisikia. Yaani wiki hii hatuna "mood" ya kuifanya hiyo kazi au kitu tunaacha. Tunasubiri siku "mood" ikipanda tukiwa na amsha amsha ndipo tufanye kazi.  

Hiyo kitaalamu tunaita kugusa kazi juu juu huwezi kuifanikisha. Na hii imekuwa changamoto kubwa kwetu. Imesababisha malalamiko kwa wengi wetu. Oh sioni maendeleo ya kazi yangu.Oh mimi nina bahati mbaya. Nataka niamie mjini huku kijijini wananichezea. Huku mjini siku hizi pamoto sioni matokeo. Mme/Mke, mpezi, bosi kabadilika. Ikumbuke hii, "huwezi kupata kama utafuti".

Kumbe; wewe mwenyewe ndiye unayejikwamisha. Kazi au kitu chako unakigusa juu juu alafu unategemea kukifanikisha kwa kiwango kikubwa. Ni ngumu sana. Hata jua litelemke bila kukifanya kitu au kazi yako kwa ubora wa hali ya juu hutofanikiwa. Ndio maana Wakolosai 3:23-24 inasema

"Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu". Maandiko yameweka wazi. Fanya kwa moyo wako wote. 

Upo shuleni, unasomea mtihani. Huwezi kuwa na ufaulu mkubwa. Maana hujakaa kwenye mchakato sahihi kiusomaji. 

Upo kazini, unasubiri hadi bosi awepo ndipo unakuwa na ari ya kazi. Hapo sahahu ufanisi. 

Upo nyumbani unasubiri shinikizo la Mume au Mke sahahu maendeleo. 

Upo kwenye mahusiano ubasubiri kila mpango utoke kwa mtu fulani. Hiyo ngoma ni nzito. Utachelewa sana.  

Ukifanya kitu au kazi kutoka ndani yako bila kuchoka lazima ifanikiwe. Hapo hakuna miujiza. Ni kazi na matokeo. Iwe wakati wa jua au mvua ifanye kazi yako au kitu kwa upendo mkubwa. Huwezi kujua nani anaenda kuwa mfano kutokana na kazi yako. 

Usisubiri watu waje kukupa hamasa katika kufanya kazi au kitu chako. Jipe hamasa mwenyewe maana ndiye unayejua safari yako. Mungu atakubariki sana. Ifanye kazi yako kwa uwezo wako wote, upendo wako wote na kwa moyo wako wote. Hakika itakuheshimisha. 


Imeandaliwa na Lackius Robert 0767702659

#10mwangaza 2023